BEKI wa kati
mkongwe wa Yanga, Kelvin Yondani, ametoa maoni yake kuhusu aina ya usajili
ambao mabosi wake wanatakiwa kufanya ili kuhakikisha wanakuwa na kikosi bora
kuelekea msimu ujao.
Tayari wapo
baadhi ya wachezaji wanaotajwa kutakiwa na Yanga katika kuelekea msimu ujao ambao ni Mussa
Mohamed kutoka Nkana FC, Heritier Makambo (Horoya AC), Tuisila Kisinda (AS
Vita), Michael Sarpong (Rayon Sports), Yassin Mustapha (Polisi Tanzania),
Bakari Mwamnyeto (Coastal Union) na Abdulhalim Humud (Mtibwa Sugar).
Yondani anasema katika usajili ujao, safu ya ushambuliaji inapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza
kwa kuletwa washambuliaji wenye uwezo mkubwa wa kufunga mabao kwani hivi sasa wanacheza vizuri, wanatengeneza nafasi nyingi, lakini changamoto inayowakabili
ni kushindwa kutumia nafasi hizo kufunga mabao ipasavyo.
Aliongeza
kuwa, pia timu yao inahitaji kiungo mwingine mmoja wa pembeni atakayesaidiana
na Mghana, Bernard Morrison.
“Timu
tuliyokuwa nayo siyo mbaya, lakini tatizo linalotukabili ni safu ya
ushambuliaji, tumekosa washambuliaji hatari waliokuwa bora na uwezo mkubwa wa
kufunga mabao.
“Ninaamini
kama mabosi wangu wakifanyia kazi hilo kwa kusajili washambuliaji na viungo
bora wa kutokea pembeni nina matarajio makubwa ya timu yetu msimu ujao kuwa
tishio zaidi.
“Hizo ndiyo
sehemu zinazotakiwa kufanyiwa maboresho lakini siyo kusajili wachezaji wengi
katika timu watakaokuwa hawana faida yoyote,” alisema Yondani.
Safu ya
ushambuliaji ya Yanga hivi sasa inaongozwa na David Molinga ‘Falcao’, Yikpe Gnamien,
Ditram Nchimbi na Tariq Seif.
Yanga ikiwa imefunga mabao 31 katika
Ligi Kuu Bara msimu huu, washambuliaji wake wanne wamefunga jumla ya mabao 13. Molinga
(8), Yikpe (1), Nchimbi (2) na Tariq (2).
SOURCE: SPOTI XTRA
umemtaja mwamnyeto pekee ktk nafasi ya ulinzi, kuliko kuongeza washambuliaji basi ulinzi upewe kipaumbele au vyote kwa pamoja
ReplyDelete