August 11, 2020

 


DIRISHA la usajili kwa timu za Ligi Kuu Bara, Ligi Daraja la Kwanza, Ligi Daraja la Pili na Ligi Kuu Wanawake Tanzania Bara, limefunguliwa tangu Agosti Mosi, mwaka huu.

 

Tangu kufunguliwa kwa dirisha hilo, kumekuwa na fujo nyingi za usajili kwa kila timu kuona inaimarisha kikosi chake kwa msimu ujao wa 2020/2021.

 

Timu za Ligi Kuu Bara ndizo zimeanza fujo hizo kwa kasi, Simba, Yanga na Azam ndizo zimekuwa zikitajwa sana katika usajili tangu kufunguliwa kwa dirisha hilo kubwa ambalo linatarajiwa kufungwa Agosti 31, mwaka huu.

 

Katika usajili huo, tumekuwa tukisikia mengi ikiwemo kuzidiana kete katika kuchukua wachezaji.

 

Kipindi hiki cha usajili ni muda ambao timu zinatakiwa kuwa makini sana kwani ukikosea tu, basi utateseka kipindi kijacho wakati ligi imeanza.

 

Mara kadhaa tumeona timu zikifanya usajili wa wachezaji wengi kipindi cha usajili, lakini wachezaji wale wanashindwa kuendana na mfumo wa timu, mwisho wa siku wanaachwa.

 

Kusajili ni jambo moja na kusajili kwa malengo ni jambo la pili. Hivyo nawaasa fanyeni usajili kwa malengo, siyo mnasajili kwa kushindana tu mwisho wa siku mnafeli.

 

Kila timu inafahamu mapungufu yao kutokana na kile ambacho walikifanya msimu uliopita. Hivyo basi sajilini kulingana na mapendekezo ya mabenchi yenu ya ufundi.

 

Itapendeza kuona usajili unaofanyika ni kwa mujibu wa mabenchi ya ufundi na si kwa mujibu wa viongozi kwani tumeona mara kadhaa wachezaji wakisajiliwa kwa matakwa ya viongozi.

 

Kocha anatoa mapendekezo yake, lakini viongozi nao wanakuwa na mapendekezo yao, mwisho wa siku wale wachezaji wa viongozi wanashindwa kwenda na mfumo wa kocha, timu inafeli.

 

Tunataka kuona msimu ujao kila timu ikiwa na wachezaji ambao wana matumizi nao, siyo kujaza tu wachezaji halafu hawatumiki, hiyo si sawa kabisa.

 

Kuwa na lundo la wachezaji halafu huwatumii, hiyo inakuja kuleta shida huko mbele kwa kuhitajika kuwalipa halafu klabu inaona kama inatupa fedha bure. Sajilini kwa malengo na siyo kwa kukomoana.

 

Kwa namna ambavyo msimu wa 2019/20 ulivyokuwa, sidhani kama kutakuwa na timu itafanya usajili ili tu kuwakomoa wapinzani, bali ni kwa malengo.

 

Azam FC baada ya kufeli msimu uliopita, imeona ijiimarishe zaidi kwa kusajili majembe mapya, Yanga nao hivyohivyo, bila ya kuwasahau mabingwa Simba.

 

Usajili wa timu zote sina shaka nao, lakini wasiwasi wangu ni kwamba, mnasajili kulingana na kile ambacho makocha wanahitaji au ni matakwa yenu viongozi?

 

Kumbukeni msimu unakuwa na mechi nyingi, kucheza mechi 34 ukiwa na wachezaji wa viwango vya chini mwisho wa siku mnaambulia maumivu makubwa.

 

Si mmeziona timu ambazo zimeshuka daraja, nyingi zimeponzwa na udhaifu wa vikosi vyao na hata Azam na Yanga zimeshindwa kushindana na Simba kutokana na kuwa wadhaifu kiviwango.

 

Yanga ilisajili wachezaji takribani 20 wapya kwa msimu uliomalizika, cha kushangaza pia ikawaacha wengi ambao walicheza nusu msimu tu. Kuanzia dirisha kubwa, ilipofika dirisha dogo wakawaacha. Huu ni upotevu wa fedha bure.

 

Binafsi nahitaji kuona kila timu ikisajili wale wachezaji ambao itawatumia. Kama mmeruhusiwa timu kuwa na wachezaji 30, si lazima mjaze nafasi zote ilimradi tu, wekeni malengo.

 

Unaweza kuwa na wachezaji wako 25, lakini wote wana uwezo wa kucheza kwa kiwango kikubwa, hapo mtafanikiwa.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic