November 10, 2020


 

WANASEMA mfungwa hachagui gereza na ule msemo wa mkulima hachagui jembe, hii haina tofauti na harakati za kijana wa Kitanga, Salim Jengo Mtango.


Mtango mwenye umri wa miaka 25 lakini hajawahi kukata tamaa ya kimaisha kutokana na kufanya kazi nyingi kabla ya kuingia katika mchezo wa ngumi za kulipwa licha ya mengine kuendelea nayo hadi sasa.


Kirekodi bondia huyo mwenyeji wa Makorora, amecheza jumla ya mapambano 16 akiwa ameshinda 13 kati ya hayo  nane kwa KO, amepigwa mapambano matatu kati ya hayo moja kwa KO.


Achana na rekodi zake na ule ufundi wake akiwa kwenye ulingo lakini tayari anashikillia mikanda kadhaa ya ubingwa aliyofanikiwa kuitwaa tangu alivyoanza mchezo wa ngumi.


Huenda akawa pia hajulikani sana lakini kwa Tanga, Mtango anapendwa na kukubalika zaidi kutokana na ukaribu wake pamoja na maisha yake ya kujichanganya katika kazi mbalimbali licha ya ubondia wake.


Bondia huyo ambaye anajiandaa na pambano lake la kimataifa dhidi ya Eduardo Mancito kutoka Ufilipino ambalo linatarajia kupigwa Novemba 28, mwaka huu kwenye Ukumbi wa Next Door uliopo Masaki jijini Dar chini ya udhamini wa Gazeti la Spoti Xtra, +255 Global Radio, DSTV, Plus TV, Kebbys Hotel, Clouds Fm na kinywaji cha Smart Gin.


Championi ambalo lilipiga kambi katika jiji la Tanga na kuweza kumshuhudia bondia huyo akijishughulisha na uuzaji wa Pweza nyakati na usiku pamoja na masuala ya uvuvi ndani ya bahari ya Hindi licha ya kupanda ulingoni kupigana.


Wenyeji wa Tanga wanaeleza kuwa kijana huyo hachagui kazi kwani pia alishawahi kuhusika na uuzaji wa dagaa wa mchele maarufu zaidi kwa watu wa ukanda wa Pwani kama Uwono katika soko la Makorora.



Mtango mwenyewe anasema ameshafanya kazi nyingi kwa lengo la kutafuta pesa kwa ajili ya kuendesha  kazi zake.


“Nafanya mambo mengi, bodaboda naendesha, shughuli ya kusajili laini nimefanya hata hapa kwenye soko la Makorora nimeuza sana samaki wabichi huko nyuma.


“Sasa hivi bado nauza Pweza, wapo vijana ambao wananisaidia kwa sababu ya ratiba yangu kuwa ngumu hasa upande wa mazoezi.


“Ninachofanya asubuhi huwa naenda mazoezini, kisha nikirudi naenda kukusanya Pweza, nawaachia vijana wanaanda kwa ajili ya biashara jioni.


“Nikitoka hapo nitaenda kwenye kijiwe cha kahawa kucheza drafti na kuongea, huwa naenda kucheza mpira, namudu kucheza nafasi ya kipa, namba 11 na beki wa kushoto bila ya shida.


“Baada ya mizunguko hiyo ndiyo narudi kwenye kuuza Pweza kwa lengo la kuwasaidia vijana majukumu yao na hiyo imekuwa kawaida kwa kuwa mimi ni mtu wa watu."


Baada ya maongezi hayo siku ya pili, bondia huyo alitupeleka katika eneo la  ufukwe wa Sahare ambapo kuna bandari ndogo ya wavuvi  na sehemu ambayo alikua akifanya shughuli zake za uvuvi. Championi liliweza kuhushuhudia namna alivyokua akifanya mambo mbalimbali akiwa baharini.

Nimeambiwa wewe ni mvuvi?


“Hawajakudanganya kweli mimi ni mvuvi, nafanya shughuli hizo japo sasa wazee hawataki niende kule kwa sababu wanasema nimepata kazi yenye uafadhali.


“Lakini kwenye kuvua nimevua na hadi leo navua, nakumbuka siku ya kwanza katika kuvua tulienda sehemu mmoja inaitwa Deep Sea hapahapa, Tanga, tulivua lakini tuliambulia 500 kila mmoja wetu kwa ajili ya chai kwa kuwa hali haikuwa nzuri.

 Kitu gani huwezi kusahau ndani ya bahari?


“Unajua mara ya kwanza kwenye kuvua nilifika Kasera huko nikaomba lifti katika vyombo vya wavuvi wengine hadi Kenya, huko nikavua sana sasa wakati tunarudi tulikutana na dhuruba kali kiasi mawimbi yalikuwa yanafunika jahazi, sisi wavuvi wote tukaingia ndani ya jahazi kujificha juu akabakia nahodha peke yake.

“Kiukweli ilikua ni Mungu  maana nilikua nahisi ndiyo mwisho wetu na tukio lingine lilikuwa ndani ya bahari, nahodha wachombo alinitukana kisha akanipiga kibao kwa kuwa nilikosea kuvuta kamba  ya nyavu, ukweli nilimrudishia kwa kumtandika ngumi tatu kwa sababu hakutakiwa kunitukana.

“Lakini baada ya hapo ikabidi niombe lifti kwenye chombo kingine kurudi nchi kavu na hapo ndiyo nikaanza kuacha kwenda baharini lakini katika kuvua nipo sawa kabisa,” anasema  Mtango.  

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic