April 1, 2021




TUNACHOTAKIWA kwa sasa kukifanya ni kumuombea Rais John Magufuli apumzike salama kwa kuwa mwendo ameumaliza.

Uwepo wake duniani na kuondoka kwake ni somo kwetu pia tunapaswa kujua kwamba ni lazima nasi tufanye matendo mema ili kuacha alama.

Kazi ambayo imebaki kwetu ni kuendeleza yale maono ambayo alikuwa anayafikiria na kuyatendea kazi. Hakuna wa kumlaumu kwa sasa kwa kuwa kazi ya Mola haina makosa.

Wengi wanaumia kutokana na kuondoka kwake. Hilo ni kweli kwa kuwa alikuwa ni mtu wa watu na anapenda kufanya kazi kwa wakati na kwa umakini.

Haivumiliki kwa namna ambavyo Watanzania wamekuwa wakimlilia kwa huzuni ila imetokea jambo ni moja kwa sasa kumuombea apumzike salama mwendo ameumaliza.

Kwa timu ambazo bado hazijawa na mwendo mzuri ni muhimu kwa sasa kufanya kazi ya kurekebisha makosa ambayo wameyafanya.

Miongoni mwa vitu ambavyo alikuwa anapenda Magufuli ni kuona matokoe mazuri kwa timu zetu zote zikiwa uwanjani kwenye mechi zake za ushindani.

Alipokuwa akipata nafasi ya kwenda uwanjani alikuwa anaheshimu wito ambao anapewa na kuhudhuria uwanjani na kuacha majukumu yake kwa muda.

Utendaji kazi wake unaonekana na hauhitaji kuanza kuuzungumzia kwa sasa kwa kuwa mengi aliyofanya yameonekana na yataendelea kukumbukwa.

Kazi kwa timu zote pamoja na wamiliki ni kuangalia namna ya kuenzi aliyoyaacha Magufuli kwa vitendo. Hakuna kingine cha kufanya ambacho kitakuwa ni heshima kwake zaidi ya kufanya yote kwa umakini na juhudi.

Ikumbukwe kuwa alikuwa anapenda kuona timu za Tanzania zinaweza kutwaa kombe la Afrika. Ni deni kwa timu zote kuweza kutimiza agizo hili.

Namna ambavyo Watanzania wanavyopenda michezo ilikuwa hivyo kwake pia. Hakuishia kufuatilia Bongo pekee bali hata nje ya nchi alikuwa anafuatilia.

Magufuli alikuwa anajua kuhusu Barcelona ile ya Lionel Messi alikuwa anajua maumivu ya timu ya taifa ya Tanzania kupoteza, alikuwa anajua ngumi alikuwa anajua riadha na michezo yote alikuwa anafuatilia.

Kwa maana hiyo ni kazi kwa kila mwanafamilia ya michezo kufanya kazi yake kwa vitendo huku akijua kwamba shujaa Magufuli alikuwa anatambua na kufuatilia michezo yote.



Alikuwa anapenda muziki iwe ni Bongo Fleva, Singeli mpaka nyimbo za dini alikuwa anafuatilia na anajua kazi za sanaa ambazo zilikuwa zinafanywa na watu wake.

Ni deni ametuachia Watanzania kuyafanya yote kwa vitendo ili kuweza kuendeleza maono yake ambayo alikuwa akiyafikiria enzi za uhai wake.

Wakati huu pia ni muda wa kuangalia hesabu kwa timu ambazo zipo kwenye hatari ya kushuka daraja kwa msimu huu wa 2020/21.

Kazi kubwa ambayo inabidi ifanyike ni kuongeza juhudi na kufanya kazi  kusaka pointi tatu. Mzunguko wa pili ushindani ni mkubwa.

Zipo timu ambazo tayari zimeonyesha nia ya kushuka daraja kwa kuwa wachezaji wameonekana kukata tamaa. Hili kwa sasa halipaswi kupewa nafasi bali kutulia na kuanza upya kupiga hesabu.

Ushindi upo kwa timu ambayo itajiandaa na kwa namna ligi ilivyo hakuna ambaye anamiliki ushindi hata akiwa nyumbani anaweza kupoteza.

Tumeona wazi kwa baadhi ya mechi ambazo zimechezwa ugenini, timu zinapata matokeo tofauti na ilivyokuwa zamani. Pia zamani kulikuwa na ubabe mwingi kwa mechi za nyumbani.

Wakati huu imekuwa tofauti ule ujanjaujanja hauna nafasi na kila timu inapata ushindi kutokana na maandalizi ambayo yamefanywa kabla ya mchezo.

Inamaanisha kwamba kila timu ambayo itafanya maandalizi mazuri kabla ya mchezo husika ina nafasi ya kushinda kwa namna yoyote.

Basi hicho kinahitajika muda wote na itafanya wachezaji kuanza kupata ushindi ndani ya dakika 90 ambazo watakuwa uwanjani kuwakilisha timu zao.

Ni mzunguko ambao kila timu inapambania malengo yake kuweza kupata ushindi. Inawezekana kwa kuwa kila mmoja anapambania ndoto zake.   

Jambo la msingi ni kuona kwamba mzunguko huu wa pili yale makosa ambayo yalikuwa yanafanyika yanapunguzwa ama kuachwa kabisa.

Waamuzi nao pia wana kazi ya kutimiza majukumu yao kwa umakini. Sheria 17 za mpira zitumike katika kusimamia ushindi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic