June 4, 2021

 

 


“KWANGU kumbukumbu mbaya zaidi ni ile ya mwaka 2003 ambapo nilikosa mkwaju wa penalti dhidi ya klabu ya Santos ya Afrika Kusini, katika mchezo wa mtoano wa Ligi ya Mabingwa Afrika licha ya kwamba tulifanikiwa kuendelea mbele.

 

“Tulisonga mbele kwa kuwa Santos nao walikosa penalti, lakini tukio hilo liliniacha katika hali ngumu sana kwa kuwa nilihisi nimeifelisha timu yangu.” Anaanza kufunguka mshambuliaji wa zamani wa kikosi cha klabu ya Simba na Taifa Stars, Madaraka Selemani ‘Mzee wa Kiminyio’

 

Nyota huyo ambaye alipata mafanikio makubwa katika soka la ndani na nje ya Tanzania kwa miaka ya kuanzia 1984 hadi 2005 kupitia Championi Ijumaa, amefunguka mambo mengi kuhusu maisha yake ya soka kama ifuatavyo;

 

Historia yako kwa ufupi?

 

“Mimi ni mzaliwa wa mkoani Morogoro, lakini nimekaa sana Dar es Salaam kwa kuwa wazazi wangu ambao kwa sasa ni Marehemu walihamia miaka mingi iliyopita, hivyo makuzi yangu yalikuwa hapa Dar es Salaam.

 

“Kuhusu kucheza soka, nilianza kucheza mpira wa mtaani ambapo nilifanikiwa kucheza timu kama Sifa United, Rupia, Tambaza ya magomeni na nyinginezo nyingi, lakini katika soka la ushindani hasa kwa Ligi Kuu, nilianza na CDA ya Dodoma mwaka 1984 ambapo nilikutana na nyota kama Jamhuri Kihwelo.

 

“Mwaka 1985 nikajiunga na kikosi cha Majimaji ya Songea ambayo kwa wakati huo ilikuwa na wachezaji kama Justin Simfukwe, ambapo baada ya hapo mwaka 1989 nikajiunga na klabu ya Fanja kutoka Uarabuni.

 

“Mwaka 1994 nilirejea Simba ambapo niliwakuta nyota kama Mohammed Mwameja, Malota Soma. Kutoka Simba nilijiunga na timu inaitwa Kajimuro mwaka 2000 ambayo ni timu ya Sigara ambayo ilibadilishwa jina, nikarejea Simba mwaka 2002 na kucheza mpaka nilipostaafu mwaka 2005.

 

Kwa sasa unajishughulisha na nini?

 

“Baada ya kuachana na soka kwa sasa najishughulisha na majukumu yangu binafsi ambayo nisingependa kuyaweka wazi, lakini nashukuru Mungu ndiyo yananiendeshea maisha.

 

Vipi kuhusiana na familia yako?

 

“Mimi ni baba wa familia ya mke mmoja na watoto wawili ambao ni Mwanahenzi wa kike na Selemani Madaraka wa kiume, kwa upande wa mke yeye si shabiki wa soka na hana timu.

 

Kusafiri kwako kama mchezaji kuliiathiri vipi familia?

 

“Kwa kuwa masuala ya kusafiri ni jambo la kawaida kwa mchezaji, nashukuru familia yangu ilikuwa inaelewa.

 

 

 

Utofauti wa maisha kwa sasa, kulinganisha na wakati unacheza soka ni upi?

 

“Utofauti wa kuendesha maisha unatokana na namna ambavyo mtu amejipanga wakati akiwa bado mchezaji, hilo ndilo linaweka tofauti ya ugumu na urahisi wa maisha, lakini kwangu naona maisha yako vilevile tu.

 

Kikosi gani kwako kilikuwa bora zaidi wakati unacheza soka?

 

“Kikosi bora zaidi kwangu ni cha klabu ya Simba cha mwaka 1994, na kuthibitisha hili ukiangalia kikosi cha timu ya taifa cha mwaka 1994 ambacho kilishinda kombe la Chalenji pale Uganda, kilikuwa na idadi kubwa ya wachezaji ambao walikuwa wakitoka Simba.

 

“Baadhi ya wachezaji wa Simba waliokuwa kwenye kikosi hicho ni; Steven Nemes, Mwamedi Mwameja, Deo Mkuki, George Masatu.

 

Ni upi utofauti wa ushindani wa Simba na Yanga, wa zamani na sasa?

 

“Ushindani ulikuwepo tangu zamani na kilichozidisha upinzani huo ni ile hali ya Simba na Yanga kutocheza mara kwa mara kama ilivyo sasa, unaweza kukuta kwa mwaka zinacheza mara mbili pekee tofauti na sasa ambapo hukutana mara kwa mara na kupunguza ladha.

 

Mafanikio gani umeyapata katika mchezo wa soka?

 

“Mafanikio ni mengi kwa maana ya mataji mbalimbali ambayo kwa kweli siwezi kukumbuka idadi yake, lakini hata kuhusiana na mabao, unajua kwa kipindi chetu hatukuwa na utaratibu maalum ya kukusanya na kutunza rekodi, hivyo ni vigumu kukumbuka kwa usahihi.

 

Ni yupi mchezaji wako bora wa muda wote

 

“Binafsi nimefanikiwa kucheza na wachezaji wengi bora katika vikosi vya timu zote ambazo nimecheza, hivyo inakuwa vigumu kutaja mchezaji mmoja.

 

Umefanikiwa kucheza michezo mingapi ya dabi ya Kariakoo?

 

“Kwa kipindi nilichokuwa ndani ya kikosi cha Simba, nilifanikiwa kucheza michezo mingi dhidi ya Yanga, kwa hesabu za haraka ni kama michezo 15.

 

Mchezo upi unaukumbuka zaidi kwenye maisha yako ya soka?

 

“Nakumbuka michezo mingi lakini miongoni mwa michezo bora zaidi ambao naukumbuka ni ule dhidi ya Yanga ambapo nikiwa na kikosi cha Majimaji niliwahi kufunga hat-trick mwaka 1989.

 

“Nakumbuka baada ya mchezo huo mashabiki wengi wa Simba walikuja na kunibeba katika hali ya kushangilia.

 

Ishu ya ushirikina kwenye michezo ya Simba na Yanga ina ukweli?

 

“Ishu ya ushirikina siyo tu kwa Simba na Yanga, mimi naweza kisema klabu nyingi zinaamini katika ushirikina, kuanzia wakati wetu na hata sasa.

 

“Kwa upande wangu ni ndani ya kikosi cha CDA ya Dodoma na Kajimuro, ndizo timu pekee ambazo sikuwahi kuona mambo hayo.

 

Unadhani hizo imani husaidia?

 

“Kwa kuwa ile ni imani, inategemea na yule ambaye anaamini lakini mimi licha ya kuhusishwa katika mazingira ya kitimu, lakini huwa siziamini na imewahi kutokea mara nyingi mnaahidiwa ushindi na hao wataalamu lakini mnaingia uwanjani na kupoteza mchezo, japo nisingependa kuweka wazi michezo husika.

 

Unadhani TFF inakutumia ipasavyo kuendeleza soka?

 

“Wachezaji wa zamani tuko hivyo hatuwezi wote kutumiwa na Shirikisho, wapo wenzetu wanaotuwakilisha.

 

Umewahi kufikiria kujihusisha na ukocha?

 

“Unajua si wachezaji wote wa soka wanalazika kuwa makocha, wengine wanaweza kujihusisha na shughuli nyingine za kujenga taifa.

 

Unaendelea na ratiba ya mazoezi kwa sasa?

 

“Ndiyo huwa nimekuwa na kawaida ya kufanya mazoezi kila wikiendi, na mara chache siku za wiki ambako huko huwa tunacheza michezo mbalimbali ya Maveterani ambapo kwa upande wangu huzichezea timu za Mbweni Veterani na ile ya Simba Veterani.

 

Siri ya mafanikio ya Simba ya mwaka 2003 iliyowavua ubingwa Zamalek ni ipi?

 

“Siri kubwa ilikuwa ni umoja wa wachezaji, benchi la ufundi na viongozi kwa ujumla, nakumbuka kuelekea mchezo huo tuliweka kambi nchini Oman, huku pia iliongezwa nguvu ya Talib Hillary ambaye ni mchezaji wa zamani wa Simba ambaye alilisaidia benchi la ufundi kwenye mbinu za kupata matokeo na kwa kufuata mashauri yake tulifanikiwa.

 

Mchezaji gani wa kimataifa anakuvutia kwa sasa?

 

“Wapo wengi kama vile; Clatous Chama, Prince Dube, Chris Mugalu, Mukoko Tonombe na wengine ambao ni vigumu kuwataja wote.

 

Kuna kitu unajilaumu ambacho hukukifanya wakati unacheza soka?

 

“Hapana, mimi naamini kila kitu kina wakati wake sisi tulikuwa na wakati wetu na huwezi kusema kuna kitu cha ziada unachoweza kukifanya tena.

 

Una ushauri gani kwa wachezaji wa sasa?

 

“Jambo la muhimu ni kuwa, wanapaswa kujifunza kutokana na mapungufu ya wale waliowatangulia na kuhakikisha hawarudii makosa.

 

Umewahi kuhusika katika matukio ya kuuza mechi za Simba na Yanga?

 

“Niliwahi kushawishiwa kutoka Simba kwenda Yanga wakati wa mfadhili wa Yanga Marehemu, Abbas Gulamali, ambapo nilifikia hatua ya kukutana na Abbas mwenyewe na kumalizana kila kitu.

 

“Lakini kabla hatujakamilisha usajili nilibadilisha maamuzi kutokana na ishu ya masilahi na Simba kupanda dau.

 

Unalizungumziaje suala la mabadiliko kwenye klabu za Simba na Yanga?

 

“Jambo la muhimu ni kwamba mabadiliko ya mfumo ni jambo la lazima kwa kuwa mpira wa sasa ni biashara na unahitaji fedha nyingi kwa ajili ya uwekezaji ambazo ni ngumu kuzitoa kwa wanachama.

 

“Hivyo wanahitaji watu wenye nia ya uwekezaji kwa ajili ya kuweka fedha, zitakazosaidia kupata wachezaji wazuri na kuweza kuwahudumia.

 

Tukio gani huwezi kulisahau kwenye maisha yako?

 

“Miongoni mwa matukio ambayo siwezi kuyasahau kwenye maisha yangu ni lile la kupinduka na gali mwaka 1986, nikiwa na kikosi cha Majimaji wakati tunatoka Songea na kurejea Dar es Salaam.

 

“Nashukuru Mungu kwa kuwa licha ya ubaya wa tukio lenyewe, lakini hakuna aliyepata majeraha.

 

Unadhani ni sababu gani inapelekea washambuliaji wa kigeni kuwatawala wazawa?

 

“Unajua hapo sababu kubwa ni ishu ya muunganiko wa kitimu, na kwa kuwa mara nyingi klabu za Simba na Yanga ambazo huwa na muunganiko mzuri wa kitimu huleta nyota wa kigeni ambao ni bora, hali hiyo imekuwa ikichangia kwa kiasi kikubwa.

 

“Lakini naamini Bocco akipewa nafasi katika michezo iliyosalia, na kwa kasi yake ya sasa anaweza kuibuka mfungaji bora kutokana na ubora wa kikosi chao, licha ya kwamba Dube anaongoza.

 

 

 

 

 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic