March 18, 2013


SOKA ina nguvu kuliko hata taasisi kubwa duniani, ndicho kinachoonekana kuendelea hapa nyumbani. Wakati uchaguzi wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF) ulipoanza kupitia michakato yake, mambo yakawa hovyo tokea wakati huo.

Nasema hovyo kwa kuwa nimewahi kuelezea namna ambavyo ukabila na udini ulivyoingia katika uchaguzi huo, kwamba kuna watu wamekuwa wakifanya kampeni zao kwa kutumia mambo hayo mawili.

Kwa wanaokumbuka nilikemea na kuelezea athari zake, lakini nilieleza uchaguzi uliomungiza Tenga madarakani nilivyoufuatilia kwa karibu namna udini na ukabila ulivyokuwa tatizo na athari zake.

Wiki iliyopita, nikachambua namna waandishi tunavyojidhalilisha kupita kiasi kuhusiana na suala la kuchambua mambo yaliyojitokeza kisheria. Hata kama hatujui lakini tumekuwa tukilazimisha tu kwa kuwa tunaamini ukiwa mwandishi basi unajua kila kitu.


Nikashauri ni lazima tujifunze, tukubali kuuliza na kupata mambo ambayo ni muhimu ili kujaziliza uchambuzi weyu. Pia niliwaasa watangazaji wa redio ambao hawana taaluma ya uandishi lakini wanajiita waandishi na kuchambua ili mradi tu kwenye vituo vya redio ili kuwaridhisha watu fulani.

Lakini leo kuna kitu kingine kimekuwa kinaendelea kujitokeza kwa kasi, kitu hiki sidhani pia kama kipo sahihi na ninaona ni sehemu kubwa ya vyombo sasa imeingia uko.
Mwandishi wa michezo unapokutana na wadau mbalimbali wa vyombo vya habari wanataka kujua wewe uko upande gani, eti wewe ni wa Malinzi au Nyamlani. Au inawezekana mtu ukakutana naye na moja kwa moja akaeleza kuwa wewe uko upande fulani.

Juzi nilikutana na rafiki yangu, mdau mkubwa tu wa mchezo wa soka na anashiriki vizuri kwa ukaribu kabisa na mchezo huo nchini. Alichonieleza eti mimi ni wa Nyamlani, tena akasisitiza watu wote wanasema hivyo.

Sikuona sana kama nina sababu ya kujitetea, huenda ningeweza kuwa na chaguo lakini sina sababu ya kufanya hivyo kutokana na mambo mawili makubwa.
Kwanza hata nikimtaka mtu sina uwezo wa kumpigia kura ashinde, lakini pili na muhimu zaidi nataka kuendelea kuwa mwandishi makini ikiwezekana zaidi ya hapa, najua sijafikia kuwa makini kuliko wengine wote duniani.

Hivyo siwezi kuwa na makundi, sitaki kuendekeza ushabiki na ndiyo maana siwezi kuwa mpambe wa Malinzi au Nyamlani. Nashukuru Mungu, pamoja na kufahamiana na kuheshimiana na watu hao hao wawili, hakuna hata mmoja amewahi kunifuata tokea kuanza kwa uchaguzi na kuniomba niwe mpambe wake kama ilivyo kwa wengine.

Labda nimewasaliti? Kwa kuwa ni watu tunaoheshimiana sana, nawaheshimu kama kaka zangu. Hawajawahi kunivunjia heshima hata siku moja na wala sioni shida mmoja wao kama atakuwa Rais we TFF kwa mujibu wa sheria.

Lakini kamwe siwezi kuwa mpambe wao, wako ambao wamekuwa wakieneza majungu wakiwemo waandishi ili kujijengea mazingira mazuri ya kuwa wapambe bora karibu ya Nyamlani au Malinzi. Sina nafasi na muda hauniruhusu kufanya hivyo.

Naweza kumsaidia Nyamlani au Malinzi, yoyote atakayekuwa tayari atapata msaada wangu, kama watataka kueleza kitu kupitia gazeti ninalolitumikia, basi mara moja nitafanya hivyo kwa kuwa ninajua Watanzania wanataka kuwasikia na ndiyo kazi yangu.

Nafanya kazi kwa ajili ya wasomaji wa Championi na si nafsi na mapenzi yangu, sijifurahishi, nafanya kitu ambacho nataka kitazamike na kukubalika miongozi mwa wasomaji ambao ndiyo wenye gazeti hili.

Salamu kwa Nyamlani na Malinzi, huo ndiyo msimamo wangu. Lakini pia salamu kwa wapambe wenu wanaoneza maneno yasiyokuwa na uhakika ili kupata ‘kitu kidogo’ kwa ajili ya kuendesha maisha yao, hakuna nafasi kwa Saleh Ally kuwa mpambe.

Nafanya kazi, hii ndiyo kazi yangu. Kwenye uandishi wa habari sipiti, ndiyo kazi yangu na sijaingia kuifanya kwa kuwa nilikwama sehemu. Nilikuwa nina ndoto nayo, naifanya kwa moyo mkunjufu na kama mafanikio yatapatikana tu.

Wapambe fanyeni kazi zenu, acheni kugeuka makalani na kuendeleza vita ya kudidimiza soka ya Tanzania. Tumbo huwa halilidhiki, njaa huwa haishi hadi mwisho wa maisha, angalieni isiwapeleke kubaya. Natumia neno njaa kwa kuwa siamini kama mtakuwa na mapenzi kupindukia na Malinzi na Nyamlani bila ya kujali nafsi zenu. Tuupende kwanza mpira wa Tanzania na kusaidia maendeleo yake.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic