Katika hali isiyokuwa ya kawaida mashabiki wa Yanga walimzomea kipa namba
moja wa timu hiyo Ally Mustafa ‘Barthez’ wakati akionyeshwa kupitia runinga
iliyokuwa ikirusha matangazo kwenye Uwanja wa Taifa, Jumanne wiki hii.
Barthez alionyeshwa wakati anapasha kwa ajili ya kujiweka fiti ili kwenda
kuchukua nafasi ya kipa Deogratius Munishi ‘Dida’ aliyeumia kwenye mechi dhidi
ya Mgambo Shootings, ndipo kamera zilipommulika na mashabiki kuanza kumzomea.
Hata hivyo kipa huyo aliendelea kupasha na kupuuzia kelele hizo za
mashabiki wa Yanga, ambao wanalalamikia wakidai uwezo wake umeshuka kutokana na
kushindwa kuzuia mabao yaliyofungwa katika mchezo dhidi ya Simba, wiki mbili
zilizopita na kutoka sare ya 3-3.
Lakini hata hivyo Barthez hakuingia kucheza mechi hiyo kutokana na Dida
kutibiwa na kuendelea na mchezo ambao walifanikiwa kushinda kwa mabao 3-0.
Alipoulizwa Razak Siwa ambaye ni kocha wa makipa wa timu hiyo, alisema: “Mimi
siwaangalii mashabiki, kikubwa yeye mwenyewe aendelee kufanya mazoezi zaidi na kuachana
na kelele hizo mashabiki. Hali hiyo ni ya kawaida kwa mchezaji yeyote.”
Aidha, Kocha Mkuu wa Yanga, Ernie Brandts alisema alichukizwa na tukio
hilo. “Sikupenda tabia ile iliyoonyeshwa na mashabiki, hawakumfanyia kitu
kizuri, nafikiri walitakiwa kumsaidia kwa kumpa moyo au hata kumshauri kama
wakipata nafasi siyo kumzomea,” alisema Brandts.
0 COMMENTS:
Post a Comment