Kipa wa Gor Mahia ya Kenya, Ivo
Mapunda amesema kitendo cha Simba kumpa ajira Kocha Zdravko Logarusic ni jambo
muhimu kwa kuwa kocha huyo ana uwezo mkubwa wa kufundisha.
Ivo ambaye sasa yupo nchini kwenye
kambi ya kikosi cha Kilimanjaro Stars, kinachojiandaa na Kombe la Chalenji, aliwahi
kufundishwa na Logarusic katika timu ya Gor Mahia.
Amesema Logarusic, raia wa Croatia,
anaweza kuisaidia Simba kwa kuwa aliwahi kuisaidia Gor Mahia kutoka nafasi ya
kumi katika msimamo wa Ligi Kuu Kenya na kuipeleka mpaka nafasi ya pili, ambapo
ilisalia kidogo timu hiyo iwe bingwa.
“Niseme ule ukweli kwamba Simba
imepata kocha bora kwa hadhi yao, kwa kipindi cha miezi sita niliyokaa naye pale
Gor (Mahia), kilitosha kuuelewa ubora wake kwa kazi aliyoifanya pale,” alisema
Ivo na kuongeza:
“Kwanza sifa moja kubwa aliyonayo Logarusic
ni kupenda kuona timu yake inashinda, hapendi kupoteza mechi, sasa hapo ndipo
wachezaji wa Simba wanatakiwa kujiandaa na hilo, lakini ukweli ni kwamba ni
kocha mzuri na yupo makini sana.”
Wakati huohuo, imefahamika kuwa kocha
huyo mpya ameomba mkataba wa miezi sita kwa lengo la kumalizia duru la raundi
ya pili.
Aidha, Kocha wa Taifa Stars, Kim
Poulsen amesema Mapunda ameonyesha uwezo wa juu licha ya kuwa amemuita kikosini
hapo kwa mara ya kwanza tangu alipoanza kuinoa timu hiyo.
0 COMMENTS:
Post a Comment