Katika hali isiyokuwa ya kawaida,
Mwenyekiti wa klabu ya Simba Ismail Rage amewapanga mashabiki na wanachama wa
timu hiyo kwa ajili ya kumshangilia.
Utafikiri kocha wa timu fulani aliyekuwa anapanga fomesheni ya 4-4-2 au 4-3-3 katika ushambuliaji, naye akaamua kuwaelekeza mashabiki namna watakavyomshangilia wakati anatoka kwenye chumba baada ya mkutano na waandishi kwenye makao makuu ya klabu hiyo.
Tukio hilo la aina yake lilifanyika
kwenye Makao Makuu ya klabu hiyo yaliyopo Msimbazi jijini Dar es Salaam mara
baada ya kumaliza mkutano na waandishi wa habari.
Mwenyekiti huyo, akisubiliwa na kundi
kubwa la mashabiki hao nje ya ofisi hiyo ya Simba, alionekana na kusikika
akiwapanga kwa ajili kumshangilia.
Rage alimuita pembeni mmoja wa komandoo
na kumtaka ashuke kutoka ghorofani haraka na kwenda kuwaambia mashabiki
wajiandae kwa ajili ya kumshangilia akiwa anatoka mjengoni hapo.
Mwenyekiti huyo alisikika akiwaambia
waandishi wa habari kuwa “Mnataka mnione nikiwa nashangilia na mashabiki basi
subilini muone ntakavyoshangiliwa.
“Anzeni nyie waandishi wa habari kuanza
kushuka chini mkiwa na kamera zenu muone nitakavyoshangaliwa, ndiyo muamini
kuwa napendwa,” alisema Rage.
Waandishi bila kujali, haraka wakashuka
chini na kukuta kundi la mashabiki waliokuwa wanamsubili mwenyekiti kwa shauku
kubwa kwa ajili ya kumshangilia.
Mara baada ya kushuka chini alipokewa na
mashabiki hao kwa shangwe kwa kumpa mikono na wengine kumnyooshea wakimpongeza
wakimtaka kuendelea madarakani.
Aliposhuka chini alisimama kama dakika
tano kwa ajili ya kuzungumza na mashabiki hao na baadaye kuelekea kwenye gari
aina ya Toyota V6 Granvia lenye namba T 300 CPR.
Baada ya kuingia kwenye gari alifungua
dirisha la juu la gari hilo na kusimama na kuwapungia mikono mashabiki hao
waliosikika wakiimba Simba! Simba! Simba! Simbaaa! Kwa sauti kali hadi gari
hilo linaoondoka likisukumwa na kundi hilo.
0 COMMENTS:
Post a Comment