December 24, 2013




Takwimu zinaonyesha kikosi cha Manchester City ndiyo hatari zaidi kuliko vingine vyote vya Ulaya katika kipindi hiki.


Timu hiyo ya England chini ya Manuel Pellegrini, kimekuwa na kazi kubwa ya kushinda kwa idadi kubwa ya mabao kuliko timu nyingine yoyote.

Safu ya ushambuliaji ya Manchester City ndiyo kali zaidi kuliko zote za Arsenal, Chelsea, Liverpool na hata kutoka katika ligi tofauti kama timu za Bayern Munich, Barcelona na Real Madrid.

Katika mechi nane za mwisho za Ligi kuu England ilizocheza, Manchester City imeshinda mechi sita, sare moja na kupoteza moja.
Kinachoonyesha vijana hao wa bluu bahari ni hatari ni hivi; katika mechi zao tano za mwisho, wamefanikiwa kufunga mabao 16, kitu ambacho ni nadra sana kutokea katika ligi za soka.

Katika mechi hizo, wamekuwa na idadi kubwa ya mabao waliyoshinda bila ya kujali walicheza na timu maarufu au la.
Moja ya mechi hizo ni ile ya Desemba 14 waliyoichapa Arsenal mabao 6-3, halafu wakamaliza hasira zao kwa Fulham kwa kuichapa mabao 4-2.

Katika mechi hizo tano, Manchester City ni mechi moja tu ambayo walifunga mabao chini ya matatu baada ya kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Southampton.
Lakini kabla ya hapo na baadaye, walikuwa wanapiga kuanzia bao tatu kusonga mbele, kitu ambacho ni nadra kwa timu nyingi za Premiership, La Liga na Bundesliga.
 
England:
Kwa England, Manchester City baada ya kucheza mechi 17, tayari washambuliaji wake wametupia mabao 51 nyavuni.
Safu ya ushambuliaji ya Manchester City inaundwa na wakali wengi wakiwemo Sergio Aguero, Álvaro Negredo, Edin Dzeko, pia viungo wake wanao uwezo wa kufunga kwa wingi wakiwemo Yaya Touré, Samir Nasri, David Silva na Jesús Navas.

Wanaowafuatia kwa karibu zaidi ni Liverpool wenye mabao 42, halafu Arsenal wenye 33 na Chelsea ya Jose Mourinho 32.

Ujerumani:
Bayern ambao ni mabingwa wa Ulaya na dunia, pamoja na ukali wa fowadi yao lakini wana mabao 42 katika mechi 16 walizocheza.

Maana yake kwa tofauti ya mechi moja, hawawezi kufikia ‘muziki’ wa Manchester City katika upachikaji wa mabao. Katika Bundesliga wanaowafuatia Bayern ni Bayer Leverkusen ambao wana mabao 32 ya kufunga.

Hispania:
Mara nyingi La Liga ndiyo imekuwa ligi ambayo timu zinafunga mabao mengi sana lakini hata wao wanaonekana ‘kukaa’ kwa ‘muziki’ wa Manchester City.

Real Madrid na wapinzani wao Atletico Madrid, kila upande una mabao 46 na kufuatiwa na wakali wa zamani wa kupachika mabao, Barcelona, yenye mabao 44.

Barcelona na Madrid jana ndiyo walikuwa wanacheza mechi ya 17, hivyo wangeweza kuongeza idadi ya mabao ya kufunga wakati Atletico walikuwa wameshapiga mechi 17.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic