Kocha Mkuu wa Simba, Zdravko Logarusic,
amesema kwa sasa anaangalia zaidi viwango vya wachezaji wake vikoje katika michuano
ya Kombe la Mapinduzi na hana presha na michuano hiyo kwani anaamini timu yake
itafanya vyema kwa hatua iliyofikia.
Simba ambayo imefanikiwa kufika hatua ya
robo fainali katika michuano hiyo ya Mapinduzi baada ya kuifunga bao 1-0 timu
ya KMKM, imeonekana kubadilika kila siku zinavyokwenda mbele.
Akizungumza na Championi Jumatano, kocha
huyo alisema kwa sasa anaangalia viwango vya wachezaji wake zaidi katika
michuano hii ya Mapinduzi inayoendelea kwa sasa.
Loga alisema ni wakati mzuri kwa
kuangalia uwezo wa wachezaji wake ili asiweze kupata shida katika upangaji wa
kikosi cha kwanza katika timu hiyo ambayo ameanza kuifundisha hivi karibuni.
Aidha alisema katika michuano hii, hana
presha na kikosi chake na anashukuru kwa kikosi chake kufikia hatua hiyo ya
robo fainali ambapo anaamini timu itafika mbali japo mpira hautabiriki.
“Kikubwa kwa sasa naangalia uwezo na
viwango vya wachezaji wangu viko vipi ili kuweza kuhakikisha wanafanya vyema si
kwa Mapinduzi tu, hata katika michuano iliyopo mbele yetu.
“Sina presha, kikubwa ni kuhakikisha
timu yangu inazingatia yale ambayo wanaelekezwa ili kuweza kufanikiwa
wanapokutana na wapinzani wao katika mchezo na kuweza kufanya vyema,” alisema
Loga.
0 COMMENTS:
Post a Comment