July 18, 2014




Na Saleh Ally
WABRAZILI wanne ambao wameajiriwa na Klabu ya Yanga, ndiyo wamekuwa gumzo hali inayofanya mashabiki wa soka kutamani kuanza mapema kwa Ligi Kuu Bara ambayo imesogezwa hadi Septemba 20, mwaka huu.


Yanga imeamua kuajiri Wabrazili wanne, wawili wakiwa ni wachezaji ambao ni Geilson Santos maarufu kama Jaja, Andrey Coutinho halafu makocha ni Marcio Maximo ambaye ni bosi na msaidizi wake, Leonardo Neiva.

Uongozi wa Yanga umeamua kuboresha benchi lake la ufundi kwa kuleta makocha hao Wabrazili, lakini bado ukatoa nafasi kwa wao kuchagua wachezaji wawili ambao wanaamini watakuwa msaada kwao.

Yanga isingekuwa na uwezo wa kuwapa nafasi Maximo na Neiva kuchagua wachezaji kiwango cha wale wanaocheza Ligi Kuu Ufaransa kwa kuwa gharama zao ni juu sana.

Lakini bado inabaki palepale, Coutinho na Jaja ni wachezaji kutoka nje ya Tanzania, hivyo wanategemewa kuonyesha kitu tofauti ambacho kitakuwa changamoto.


Kuna mambo kadhaa ya kuangalia kuhusiana na wachezaji hao, lakini kwanza ni lazima kuutoa nje uongozi wa Yanga kwa kuwa usajili uliofanyika ni pendekezo la Kocha Maximo.

Suala la ujio wa Coutinho, Jaja na kupokewa kwao, hizo tayari ni historia na sasa kinachoangaliwa ni kuhusiana na suala la wataonyesha uwezo kiasi gani, msaada wao kwa Yanga na changamoto kwa soka ya Tanzania.

Miguu, macho, kichwa ndivyo vinatakiwa kuzungumza. Wabrazili hao hawatakiwi kuwa na maneno au visingizio vingi, badala yake waonyeshe kile ambacho kimewaleta hapa nchini.

Wakiisaidia Yanga kufanya vizuri, watakuwa wameisaidia soka ya Tanzania kwa kuwa matarajio ya wengi ni kwamba mchezo wa soka uko juu nchini kwao. Hata kama Brazil ilifungwa mabao 7-1 na Ujerumani katika Kombe la Dunia, si rahisi kuwafananisha na kiwango chetu.

Bado hawawezi kuwa malaika, kwamba kila watakachokuwa wanafanya kitakuwa ni zaidi ya kile ambacho kimekuwa kikifanyika hapa nyumbani. Wanayo changamoto.

Pamoja na changamoto ambayo wataipata kuonyesha walichonacho, mambo kadhaa ya msingi kwao na kwa wazalendo, ndiyo yapewe nafasi.


Uwezo:
Coutinho na Jaja lazima waonyeshe uwezo, raha ya mpira hauchezwi kwenye uwanja wenye minazi kwamba kuna mtu anaweza kujificha. Kila kitu hadharani, kama wanaweza, kila kitu kitaonekana waziwazi.

Kuwapa muda si jambo baya, angalau nusu msimu, lakini zaidi ya hapo, hakutakuwa na sababu ya kuendelea kubaki nao kama watakuwa wanacheza samba lisilokuwa na msaada badala yake lile ambalo linaburudisha watu bila Yanga kupata mafanikio.

Deni lao ni kuonyesha uwezo wao ambao ni msaada kwa Yanga, zaidi ya hapo mengine yatakuwa ni hadithi tu.

Kuzidisha:
Wao ni binadamu, wanaweza kukosea, wanaweza kufanya vibaya, hivyo mashabiki wa Yanga wana kila sababu ya kuamini hawawezi kufanya kizuri kila siku.

Hawatakuwa na vizisingizio watakapoharibu, lakini kuzidisha imani kwamba wao ni Wabrazili, hivyo watacheza kama alivyo Neymar au Oscar itakuwa ni makosa.

Kuna wachezaji wengi hapa nyumbani hawana uwezo kama wa Mrisho Ngassa au Ramadhani Singano ‘Messi’. Hivyo hilo linawezekana kwa Wabrazili hao pia, ndiyo maana wamekuja kucheza Tanzania.

Wivu:
Suala la wivu ni maumbile ya binadamu, kulikwepa asilimia mia si rahisi hata kidogo. Hivyo wachezaji wa Yanga wanaweza kuwa na wivu dhidi ya wachezaji hao.

Ikitokea kuna wale ambao wanawanyima ushirikiano hata kama kimyakimya kwa hofu kwamba wao watatamba, basi wajue watakuwa wanajiangusha wao na Yanga.

Ndiyo, inawezekana kujiangusha wao kwa kuwa wakifeli Wabrazili hao, itakuwa imefeli Yanga na mchezaji aliyewabania naye atakuwa amefeli. Kila mtu ana nyota yake, kusaidiana kwenye timu ni kuisaidia timu na kujisaidia mwenyewe, hivyo waamini ushirikiano kwa wageni hao ni jambo la kwanza kabisa.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic