January 19, 2015


MWAKA jana nilikuwa Mtanzania pekee niliyeshiriki utoaji maoni, uundwaji na uendeshaji wa taasisi maarufu ya The 1 in 11 Campaign ambayo inashirikiana na klabu ya Barcelona na Shirika la Umoja wa Mataifa la Unicef kuhakikisha zaidi ya watoto milioni 30 wa bara la Asia wasiokuwa na uwezi wa kifedha, wanakwenda shule.


Hakuna ubishi, katika dunia hii masikini zaidi wako katika mabara matatu ya Afrika, Asia na Amerika Kusini. The 1 in 11 Campaign imewakomboa wengi sana barani Asia.

Nilichangia mambo kadhaa ya kimuundo na kupewa majibu ya ahsante kutokana na nilikitengeneza kuwa ni msaada mkubwa. Lakini nilihoji vipi hakuna kitu kama hicho barani Afrika? Bado sijapata jibu.

Huenda nikasubiri jibu kwa muda mrefu bila ya mafanikio na hakuna njia lahisi ya kulazimisha hilo lifanyike. Bado macho na moyo wangu kwa kushirikiana vinaona watoto wengi wa Kitanzania hawajaenda shule licha ya kuwa na uwezo mkubwa kiakili darasani.

Wanashindwa kwenda kutokana na umasikini wa familia zao. Au wana wazazi wenye uwezo lakini si wale wanaowajali vijana wao na huenda pombe na ngono ndiyo wamezipa kipaumbele.

Nimepita katika mateso makubwa ya kukosa ada nikiwa mdogo sababu ya mirafakano ya kifamilia. Kitu kinachoniumiza nikiona Mtanzania mwenzangu pia ameshindwa kwenda shule sababu ya ada halafu bado nikawa sina uwezo wa kumsaidia.

Ninaamini kabla ya kusubiri The 1 in 11 Campaign waje barani Afrika na baadaye kufika Tanzania, basi sisi wenyewe tunaweza kujisaidia tukautumia mpira kama sehemu ya kuisaidia jamii na si kusaidia kundi la watu wachache peke yao.

Soka kuchangia kwenye jamii ni jambo zuri kwa kuwa ni mchezo wa jamii. Ndiyo maana Barcelona wanashiriki na balozi wao ni nyota Lionel Messi.

Usiseme Simba, Yanga, Azam FC, Mtibwa Sugar na wengine wanatafuta fedha hivyo hawawezi kuchangia elimu, itakuwa kichekesho.

Hata hapa nyumbani kuna tamasha la mara moja kwa mwaka, linaitwa Tamasha la Matumaini, limekuwa likichangia elimu na tayari kuna mabweni kibao yamejengwa kwa tamasha hilo.

Ndiyo maana nasema soka pia linaweza kuchangia elimu, kusaidia watoto wa wasiokuwa na uwezo au watoto wenye uwezo wasio na nafasi ya kwenda shule wakasome.
Mjadala wangu wa mapato ya mechi ya Nani Mtani Jembe kati ya Simba dhidi ya Yanga nauendeleza hapa. Kwamba zile fedha ambazo zimeyayuka kusikojulikana, basi zingeweza kusaidia kupeleka wadogo zetu wengi wakasome shule.

Kuwa na taifa la watu wengi walioelimika ni bora zaidi. Soka inaweza kusaidia, naendelea kuhoji zile fedha za Nani Mtani Jembe ni nani na nani walichukua na iliwaje?

Kuna msomaji mmoja wa Championi kutoka mkoani Morogoro ambaye alichangia kuhoji mapato hayo na ujumbe wake ukachapishwa na gazeti hili alipiga simu na kulalamika alikuwa akitishiwa na mtu aliyejitambulisha anatokea Kampuni ya Bia Tanzania (TBL).

Nikalifuatilia hilo, lakini ilionekana hakuna uhakika wa hilo na mimi nikamueleza inaonekana mtu yule hatokei TBL huenda ana maslahi yake binafsi na anataka kulitumia vibaya jina hilo.

Lakini mimi bia kuna mtu alinipigia akihoji kwamba TBL haijachukua fedha kwa nini ninaiweka kwenye mlolongo huo? Sasa ninajua waandaaji walikuwa wao, halafu hatujui fedha zimekwenda wapi! Pia sijawahi kusema TBL wamechukua, ila ninahoji na ninaona wao wanaweza wakatueleza.

Fedha zilizopatikana kwenye Mtani Jembe, Simba, Yanga, TFF na wadau wengine wangefaidika. Lakini ninaamini hata vijana wa Kitanzania wangeweza kufaidika kielimu kama ambavyo The 1 in 11 Campaign inasaidia barani Asia.  Fedha za Mtani Jembe zinaweza kuanza kusaidia na kama zimetumiwa tuambiwe ni kina nani!



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic