Na Saleh Ally
Nilikuwa kati ya wapenda
soka waliopata nafasi ya kushuhudia mechi kati ya wenyeji Coastal Union dhidi
ya wageni wao Yanga kwenye Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga.
Ilikuwa ni mechi ya Ligi Kuu
Bara kati ya timu kongwe ambazo kila moja ina rekodi ya kuwahi kutwaa ubingwa wa Tanzania
Bara.
Hakika ilikuwa ni mechi
kubwa kwa kuwa Yanga na Coastal Union ni kati ya timu za wananchi na zenye
kiwango kikubwa cha mashabiki wanaoziunga mkono.
Ingawa siungi mkono, lakini
utaona watu waliojitokeza, upinzani wao na hata wakafikia kugombana. Maana yake
kila upande una watu wake, tena wa kutosha na wenye machungu kwa timu zao.
Swali langu, Watanzania
bila ya kujali ni Tanga, Shinyanga, Mwanza au Kigoma wana mapenzi na timu zao
tu na si soka ya Tanzania?
Nauliza hivyo kwa kuwa
swali linatuhusu Watanzania wote wapenda mpira katika maeneo husika. Mfano,
nizungumzie Tanga na aibu ya Uwanja wa Mkwakwani katika mechi hiyo ya Coastal
Union dhidi ya Yanga.
Wakati tukiangalia mechi
hiyo kwenye runinga kupitia Azam TV, wengi ambao si wapenda soka walikuwa
wakiuliza maswali yanayokasirisha. Mojawapo ni hili: “Mbona uwanja una sura
mbaya hivyo, hebu angalia Afcon, kweli hamuoni vibaya kuangalia mpira mbaya
hivyo?”
Maswali hayo yalikuwa
yanakera, jibu la kwanza ni kwamba muulizaji hakuwa akijua lolote kuhusu soka.
Lakini swali lake lilikuwa limejaa ukweli mtupu.
Tangu mtu huyo alipouliza,
muda mwingi niliangalia mpira ule nikiwa najiuliza maswali mengi sana, hasa nilipoona
wachezaji wakikokota mpira.
Hakika ilikuwa hovyo
kabisa, hali haikuwa nzuri na unaweza kusema ni aibu kwa taifa letu kuwa
mipango mingi ya madai ya kuendeleza soka huwa ni hadithi za udanganyifu.
Mfano mzuri, msimu ujao,
Uwanja wa Mkwakwani kwa msimu mmoja utachezewa mechi 45 kwa kuwa kila moja
kuanzia Coastal Union, Mgambo FC na African Sports iliyopanda, zitacheza mechi
15.
Yanga, Simba, Azam FC,
Mtibwa Sugar na nyingi, kila moja itashuka mara tatu katika Dimba la Mkwakwani.
Dimba bovu kabisa na aibu kwa soka hapa kwetu nyumbani.
Katika mechi ya Coastal
Union dhidi ya Yanga, ilionekana wazi watu walishindwa hata kukokota vizuri
mpira kutokana na uwanja kujaa mabonde.
Tunataka soka liendelee, kuwe
na mchezo wa kuvutia na timu zinapigana vikumbo kusajili wachezaji ghali wa
kimataifa, lakini kwa uwanja kama huo wa Mkwakwani maendeleo yatapatikana vipi?
Ndiyo maana nikauliza,
Watanzania wanapenda timu zao tu na si mpira wa Tanzania? Maana vipi Mkwakwani
uwe uwanja mbovu kiasi hicho wakati kuna rundo la timu kwenye mkoa huo zinazoshiriki
Ligi Kuu Bara?
Inakuwaje wanaomiliki
uwanja huo, CCM, wanashindwa kutengeneza uwanja bora wa kuchezea? Vipi wananchi
wa Tanga hawapigi kelele ili kusaidia mabadiliko kwa wahusika kubanwa hadi
watengeneze uwanja?
Kelele nyingi ooh, Coastal
ya kwetu, mara ooh siyo ya kwao! Mbona hamsemi uwanja wenu ni aibu? Au hao
wahusika mbona hawapambani kuondoa aibu hiyo kwa kutengeneza uwanja bora wa
kuchezea wakati wakijua wana uwanja mbovu kabisa?
Kwa mechi 45 za msimu ujao ndani
ya Mkwakwani, ni hadithi mpya inayoendelea kuwa ya Alinacha na kamwe mafanikio
hayatapatikana.
Uwanja wa Mkwakwani katika
eneo la kuchezea ni moja ya aibu za mpira wa Tanzania kwa kuwa pamoja na
ukongwe wake, utaona Kambarage Shinyanga au Nangwanda Mtwara, ni viwanja bora
na wahusika wanajua kwamba kweli ili kucheza soka bora, lakini uwe na uwanja
bora.







0 COMMENTS:
Post a Comment