Na Saleh Ally
KOCHA wa Manchester United, Louis van Gaal,
amechukua uamuzi wa moja kwa moja kumtimua kipa Victor Valdes baada ya kukiuka
agizo lake la kutaka akacheze katika timu za vijana.
Valdes kaonyesha ni mkubwa na jeuri, lakini
van Gaal kaonyesha ni mkubwa zaidi yake, mwisho uamuzi unafuatia, mshindi
lazima atakuwa kocha huyo.
Kocha Hans van Der Pluijm ndiye alitoa
uamuzi wa mwisho wa kuachwa kwa kiungo aliyeitwa kipenzi cha Wanayanga,
Athumani Iddi ‘Chuji’. Wapo walioona alikuwa anakosea, wakasogea kumsihi na
hata viongozi wakajaribu kumshawishi ampe muda.
Msimamo wa Pluijm ukawa ni uleule, Chuji
akaondoka Yanga. Leo kuna waliopata nafasi yake wanaonekana, jiulize nani
angemuona vizuri Frank Domayo au Salum Telela lakini sasa Said Juma ‘Makapu’?
Kocha Mfaransa Patrick Liewig, mara tu maada
ya Simba kurejea kutoka Oman, akatoa msimamo wake kwamba wakongwe kadhaa,
akiwemo Haruna Moshi ‘Boban’, kipenzi cha Wanasimba hawapaswi kuendelea kuichezea
Simba.
Boban alikuwa ‘roho’ ya Wanasimba, lakini
Liewig akashikilia msimamo wake, akatoa nafasi kwa vijana wakiwemo ambao
baadaye walikuja kuwa hazina ya Simba hadi leo hii. Boban akaondoka zake na
Simba imeendelea na maisha yake na watu wamesahau.
Kocha Alex Ferguson alipata mafanikio
makubwa sana katika kipindi chake cha zaidi ya miaka 20 akiwa na Manchester
United. Lakini ukisoma kitabu chake au wale waliokifuatilia kupitia gazeti hili,
watakuwa wamejifunza mambo mengi sana.
Kwamba Ferguson amepitia milima na mabonde
na ugumu wa kazi yake haukuwa kwa mashabiki zaidi, badala yake wachezaji ambao
alilazimika kupambana nao kweli.
Mfano kuondoka kwa David Beckham, Roy Keane
ambaye hadi leo haelewani naye. Utaona lilikuwa ni suala la kushikilia msimamo
wake kama kocha kwa manufaa ya timu kwa kuwa Keane alikuwa akionyesha dharau ya
wazi kwa msaidizi wake, Carlos Quieroz akitaka ampande kichwani.
Kawaida, wachezaji wanapofanikiwa na kuwa
maarufu huwa wana mafariki wawili wakubwa. Viongozi wa klabu na mashabiki ambao
huwa wanawatetea kwa kila namna kuhakikisha ikiwezekana hata kocha afanye
anavyotaka mchezaji.
Ferguson anasema kwa kocha yeyote akiteleza
na mchezaji mmoja au wawili wakawa juu ya kichwa cha kocha, basi ajue
amekwisha!
Amekwisha kwa kuwa kazi itamshinda. Ferguson
anaamini kocha anatakiwa kuwa juu ya wachezaji wote, bila ya kujali umaarufu au
utajiri wao. Kocha ndiye mhimili, mzazi na kiongozi wa timu.
Mchezaji anabaki kuwa sehemu au mtoto ndani
ya timu. Mfano mzuri katika familia zetu za Kiswahili, mtoto mwenye uwezo
kifedha anaweza kusikilizwa na wazazi hadi kufikia kuingiza chuki au dharau.
Hapa mzazi anapaswa kusimamia muongozo sahihi bila ya kujali nani ana uwezo
upi.
Unaweza kusema misimamo ya Pluijm na Liewig
ndiyo iliyowang’oa Chuji na Boban katika vikosi vya Simba na Yanga. Hakika
angekuwa Boniface Mkwasa au Jamhuri Kihwelo ‘Julio’, wasingeweza maana kama
wangeitwa na viongozi au kupigiwa simu na mashabiki maarufu, basi wangeshindwa
kushikilia msimamo wao.
Kilichowafanya makocha hao kuwaondoa
wachezaji hao ilikuwa ni nidhamu na hakuna jambo jingine. Hawaonyeshi kujituma,
lakini muonekano wa kawaida kwamba wao ni nyota hivyo hawaguswi.
Ukiangalia hayo ndiyo mambo wanayofanya
akina Ferguson, van Gaal, Arsene Wenger na wengine wengi, jambo ambalo hata
makocha wazalendo wanapaswa kujifunza.
Kuna wakati unafikia unakiamini kitu, lakini
inakuwa vigumu sana kuwashawishi watu mapema. Ukichukua uamuzi wa kukifanya
unaweza kujikuta umebaki peke yako au na watu wachache sana wanaokuunga mkono.
Kama ni muoga utaachia njiani, lakini kama
uko thabiti, basi hutayumba na kuhofia maneno na haya ndiyo wanayofanya makocha
wengi wenye mafanikio kama ulivyoona Jose Mourinho wa Chelsea alipoamua
kuwatosa wachezaji nyota kama Juan Mata na David Luiz kwa kukubali kuwauza
halafu bado timu yake ikawa bingwa wa England.
Lakini makocha wazawa wakubali kwamba kama
wana uwezo, kujiamini na kuchukua maamuzi magumu ambayo hata kama si sahihi
leo, yanaweza kuwa sahihi baadaye, basi nayo ni sehemu ya ubora wa uwezo sahihi
na ndiyo moja ya vitu wanavyokosa, wachukue sasa ili kujiimarisha zaidi.










0 COMMENTS:
Post a Comment