Kocha Mkuu wa Simba, Dylan Kerr, amesema licha
ya kutowafahamu vizuri wapinzani wake katika mechi ya keshokutwa Jumatano,
Tanzania Prisons ya Mbeya, bado anaamini timu yake itaibuka na ushindi.
Timu hizo zitakutana katika mchezo wa Ligi Kuu
Bara mkoani hapa, ambapo Simba imekuwa ikipata wakati mgumu kila inapokuja
Mbeya kucheza, lakini kitendo cha kuifunga Mbeya City, juzi kimemuongezea
morali ya kushinda katika kipute dhidi ya Prisons.
Mara tu baada ya
mechi dhidi ya Mbeya City kwenye Uwanja wa Sokoine ambapo pia ndipo
kutakapofanyika mchezo wa keshokutwa, Kerr raia wa Uingereza alisema hawafahamu
wapinzani wake lakini amekuwa akiambiwa wana timu ngumu.
“Nimeambiwa Prisons ni timu ngumu kwa Simba,
lakini sina wasiwasi wowote, timu yangu ipo fiti na wachezaji wanaonyesha
kuzoeana na tumeshazoea mazingira ya Mbeya,” alisema Kerr.
Alisema hakuna kinachoshindikana na lengo lao
ni kuibuka na ushindi tu katika mchezo huo.
“Mbeya City wao tuliwaona kabla ya mchezo
tukawajua mapema aina ya uchezaji wao, hivyo tutahakikisha tunavuna pointi zote
sita licha ya mimi binafsi kutowajua Prisons,” alisema Kerr.
0 COMMENTS:
Post a Comment