November 9, 2015


Na Saleh Ally
SUALA la viwanja limekuwa ni sawa na gumzo la kawaida kabisa kama unazungumzia mpira wa Tanzania. Hakuna kiongozi anayeona kwamba ni jambo kubwa sana.

Kumekuwa na mazoea makubwa kwamba timu zinazoshiriki hata ligi za juu kama Ligi Daraja la Kwanza na Ligi Kuu Bara nazo zinaweza kuendelea kufanya mazoezi kwenye viwanja vya ‘kuokoteza’.

Mfano viwanja vya shule za msingi au sekondari au viwanja vingine ambavyo vinakuwa ni kwa ajili ya watoto au vijana.
Hii imekuwa ni kawaida kabisa na hali hii inaonekana kuzoeleka karibu kwa kila timu huku ikionekana timu kutokuwa na uwanja ni jambo la kawaida na si kulishangaa.

Hiki ni kitu ambacho hakionekani kuwa ni kibaya au cha hovyo kwa kuwa viongozi wengi wa soka wamekuwa wakifanya mambo kwa kulipua na wenyewe wanaona ni sawa kwa kuwa si wanaowaza kuleta maendeleo.

Kila kiongozi anaamini kulipa kiasi cha fedha ili timu yake ikafanya mazoezi ni sahihi kuliko kujenga uwanja au kutengeneza angalau uwanja wa mazoezi tu.

 Kichekesho hiki kimeendelea kuvunja mbavu kila kukicha. Viongozi wanaendelea kutembea kila siku na katika nchi mbalimbali wanakutana na changamoto za kuona kila klabu ina uwanja angalau hata wa mazoezi.

Wameona karibu kila nchi, suala la uwanja wa mazoezi ni lazima. Kuwa na klabu ya soka bila uwanja wa mazoezi kwa ajili ya timu ni kichekesho na sehemu ya kuonyesha hakuna nafasi kwa Tanzania kupiga hatua mbele kwa kasi.

 Bado viongozi wanaliona na kuliacha, ndani yake pia utasikia watu wanazungumzia suala la maendeleo ya vijana ambalo kamwe halitawezekana.

Tumeona Yanga na hata Simba wakilazimika kupunguza idadi ya mazoezi kutokana na gharama za kulipia viwanja.
Wakati mwingine makocha wamekuwa wakilazimishwa kufanya mazoezi mara moja kwa siku wakati wangependelea kufanya mara mbili.

Nakukumbusha Kocha Ernie Brandts aliyekuwa akiinoa Yanga alivyolalamika kutafutiwa magoli madogo lakini hakuyapata hadi alivyoondoka. Nakukumbusha alivyolia kuhusiana na ubovu wa viwanja kwamba anashindwa kufundisha anachokitaka kwa kuwa mpira hauwezi kutembea chini.
Tunalalamika tuna wafungaji wasio na uwezo. Tunajua pamoja na vipaji lazima kuwe na mafunzo ambayo pia vigumu kupatikana kwenye hali ya viwanja tulivyonavyo.

Jiulize katika hali ya kawaida, kwa nini tushindwe kuwa na viwanja? Tunakosa nini hasa hadi kuwa na viwanja liwe ni jambo gumu sana kiasi cha kuwa gumzo lisilokuwa na utatuzi?

Ardhi tunayo, majani yapo, hata maji yanapatikana. Hapa ni fedha za utengenezaji na mtu wa uangalizi. Sasa hili linashindikana kwa timu kama Simba. Tena ajabu zote mbili zina viwanja na kila kitu, bado majani na mtu wa uangalizi pekee?

Klabu nyingine pia zinapaswa kuliangalia hili. Ukombozi wa soka nchini bado, lakini suala la viwanja ni lazima lifanyiwe kazi na hakuna sababu ya kuwa na mzaha au viongozi kusubiri hadithi au kuendelea kukubaliana na utaratibu huu.

Inawezekana kabisa viongozi wamekubali kufeli kwa miaka yote lakini inapendeza huu wa 2015 ukawa mwisho na baada ya hapo mabadiliko yaanze na viwanja.

 Klabu zibadilike, viongozi wawe na ndoto kweli ya kuendeleza soka badala ya maneno. Tukubaliane bila ya viwanja, maendeleo sahihi ya soka yatakuwa ni hadithi tu.

 Viongozi acheni maneno mengi, kweli nendeni na program ya muda. Halafu angalieni program ya muda mrefu na tukubali hakuna mafanikio kimataifa kama tutabaki hapo tulipo na klabu zetu mataji ya Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho Afrika yataendelea kuwa ni hadithi tu.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic