Mshambuliaji wa Yanga, Amissi Tambwe amesema alikuwa na hisia lazima angefunga katika mechi ya watani, jana.
Yanga iliitwanga Simba mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kuweka rekodi ya kuifunga mechi mbili mfululizo tena zote kwa idadi inayofanana.
Tambwe aliyewahi kuichezea Simba kabla haijamuacha kwa madai kuwa haendani na mfumo wa Kocha Patrick Phiri, alifunga bao la pili jana wakati katika mechi ya kwanza, alifunga bao la kwanza.
“Nilkuwa nahisi nitafunga, nilijua makosa mengi ya Simba. Lakini sikuwa na uhakika kwa kuwa vitu vya mpira vinabadilika,” alisema Tambwe.
Alisema anafurahi kuifunga Simba kwa kuwa bao analofunga linakuwa ni msaada kwa Yanga lakini anaongeza idadi ya mabao ya kufunga.
Sasa Tambwe amepachika mabao 15 akiwa katika nafasi ya pili, anayeongoza ni Hamisi Kiiza wa Simba aliyefunga mabao 16 hadi sasa.







0 COMMENTS:
Post a Comment