Baada ya kurejea uwanjani, kiungo wa Simba, Haruna Niyonzima raia wa Rwanda amemuahidi makubwa kocha wake Pierre Lechantre kwa kusema kuwa ni nafasi nzuri kwake kuonyesha kiwango baada ya kupata nafasi ya kucheza.
Niyonzima alikaa nje ya uwanja tangu na kukosa baadhi ya mechi baada ya kuumia enka kulikomsababishia kupelekwa nchini India kwa matibabu kabla ya kurejea kikosini.
Kiungo huyo machachari alipewa nafasi ya kucheza kwa mara ya kwanza tangu arudi majeruhi katika mchezo dhidi ya Njombe Mji, Jumatatu wiki hii kwenye Uwanja wa Sabasaba, akichukua nafasi ya Shiza Kichuya dakika ya 81, ambapo Simba ilishinda mabao 2-0 yaliyofungwa na John Bocco.
Niyonzima alisema, amefurahi kuona amerejea uwanjani kwa mara nyingine baada ya kukaa nje kwa muda mrefu.
“Nimefurahi kurudi uwanjani kwa kuwa nimekaa muda mrefu nje bila ya kucheza ni hatua moja kubwa sana kwangu, naamini mambo mengine yanayokuja ni mipango ya Mungu.
“Nalishukuru benchi la ufundi kwa kuniamini na kunipa nafasi ya kucheza naamini nitaendelea kufanya vyema zaidi katika mechi zinazokuja.
“Tunahitaji kujipanga zaidi ili kushinda mechi zinazofuata kwa lengo la kutimiza lengo letu la kutwaa ubingwa wa ligi msimu huu, kila mchezaji anaonyesha nia ya kupata ushindi,” alisema Niyonzima.
CHANZO: CHAMPIONI
Chaka la Mzamiru ni dhahiri, naamini anajipanga kuja kwa kasi
ReplyDelete