AY SI BONGO TU, MPAKA MAREKANI PIA, NI BALAA
Wasanii wa Afrika ambao katika miaka ya hivikaribuni wamepata umaarufu sana na kusifika kwamba ni matajiri ni Davido na P Square. Kikubwa kilichowabeba hawa ni ubora na umaarufu wa kazi zao ambazo zimewatengenezea fedha nyingi.
Lakini hata kwenye matumizi wamezitendea haki fedha hizo. Wasanii hao wamenunua nyumba za makazi nchini Marekani na kushtua umma wa Kiafrika ambao ulidhani kwamba mambo hayo hayawezekani kutokea.
Sasa Mtanzania AY katika kuthibitisha kwamba akili yake inafikiri mbali zaidi nay eye ni wa anga za kimataifa, naye akanunua Mjengo maeneo ya Calabasas ingawa hajataka kufafanua gharama zake.
“Ni kweli nimefanikiwa kupata nyumba Calabasas na ndipo yatakuwa makazi yangu, ninamiliki nyumba mbili ikiwemo hiyo ya Marekani na moja Tanzania,na pia ninamiliki magari manne,”anasema AY ambaye aliwahi kung’ara na kundi la East Coast la Upanga Jijini Dar es Salaam.
AY ambaye ni miongoni mwa wasanii wakongwe wa Bongo Fleva na aliyejijenga zaidi kimuziki nje ya Tanzania, amezungumzia sanaa hiyo na kukiri vijana wengi wako vizuri na mabadiliko ni makubwa sana tofauti na awali. Msanii huyo ambaye alifanya ziara maalum katika ofisi za Global Group zilizoko Sinza Mori Jijini Dar es Salaam, alisisitiza kuwa Tanzania kwa sasa inafahamika kila kona kwasababu ya muziki.
“Muziki unakuwa kwa sababu vitu ambavyo tulikuwa tunazungumza siku zote kuhusu watu kufanya video nzuri na pia kutambua kwamba kipato unachokipata kwenye muziki siyo kwamba ni feva ni biashara na biashara yeyote ina taratibu zake ambayo ni kwamba huwezi kupata hela nyingi kama wewe huweki hela kwenye biashara yako,”anasema AY ambaye ameoa Rwanda.
“Kwa hiyo nimeanza kuona wadogo zetu na ndugu zetu wengine tulioanza nao muziki,wamelitambua hilo kwa sasa hivi,kwa sababu zamani ulikuwa ukimuelezea mtu alikuwa hakuelewi kwa hiyo hicho ndio kitu kinachonifurahisha na ukiona hivyo maana yake unaona muziki umekuwa.
AY akianya mahojiano na mwandishi wa Global Publishers, Neema Adrian.
“Muziki wa Kenya ulikuwa mkubwa zamani lakini kwa sasa, sisi tunafanya vizuri Afrika Mashariki yote kiasi kwamba mpaka unaona wanamuziki wa Kenya wanalalamika ooh Watanzania wanakuja huku wanachukua hela nyingi lakini kiukweli hali halisi wakati wao walikuwa wanakuja huku kufanya shoo zao mimi nilikuwa ni mmoja wa kiungo wao muhimu kukutanisha Wakenya na Watanzania.
“Kulikuwa hamna Mtanzania msanii ambaye alikuwa analalamika lakini mwisho wa siku nilikuwa nawajenga watu na kuwaambia kwamba hii ni biashara kwa lazima kuwekeza ili uweze kupata mafanikio”
Spoti Xtra:Unakumbuka nini wakati unatafuta kutoka kwenye muziki?
AY: Kiukweli sikuwahi kukata tamaa kabisa ila miundombinu ya kibiashara haikuwa vizuri zamani promosheni ilikuwa inakupromoti yeye ndio anapata faida kwa sababu mikataba ilikuwa mibovu halafu pakukimbilia huna yaani miundombinu ya biashara ya muziki ilikuwa migumu sana kwenye mfumo wa zamani.
Spoti Xtra: Je una mpango wa kuirudisha East Coast?
AY: Kuna rekodi ambayo tumeifanya na GK Kwa hiyo ikikamilika tunaweza kutangaza kwamba East Coast imerudi au la.
Spoti Xtra: Unamzungumziaje Gk?
AY: Ni kaka yangu haiwezi zikapita wiki mbili au mwezi bila kuonana na tunashirikiana.
Spoti Xtra:Mara nyingi umekuwa ukifanya muziki na Mwana FA unamzungumziaje?
AY:Yaani yule ni ndugu kabisa nafikiri maisha aliyoyapitia na mimi niliyoapitia tukisimuliana unakuta yanaendana pia watu ambao yeye anafahamiana nao na mimi nafahamiana nao kupitia njia nyingine kwa hiyo naweza kusema ni ndugu yangu na muda mwingi huwa nakuwa naye.
Spoti Xtra:Unajisikiaje kuwa mtu maarufu.
AY:Siyo jambo rahisi unajua unaenda kwenye shoo 2018 kwenye ‘bakisteji’ unakuta watu wapya halafu na wewe bado upo imara hata vijana ambao wameingia kwenye gemu bado wanaendelea kujifunza kutoka kwako.
Spoti Xtra: Unamiliki Albamu ngapi mpaka sasa?
AY:Ninamiliki Raha kamili ya 2003, Hisia zangu 2005 na Habari ndio hiyo ambayo nilishirikiana na Mwana FA 2007 na baadaye miundo mbinu ya kutoa albamu ilikuwa imegeuka tayari kwa hiyo tukasikisha kutoa albamu.
Spoti Xtra: Una nyimbo mpya kwa sasa?
AY: Ndio. Unaitwa Safari ni wimbo ambao unaelimisha na kufundisha na kuliwaza kwa wakati mmoja ni wimbo wakikubwa unaweza kusikilizwa na mtu wa rika lolote na nimetumia muda mwingi kutengeneza kwa naamini utaishi miaka mingi na nimemshirika Mzee King Kiki na nitauzindua tarehe 28 mwezi huu ni dizaini ya muziki niliofanya nikishirikiana na Sauti Sol.
Spoti Xtra: Mbona kwa Tanzania sasa tunamsikia tu Diamond na Ally Kiba inakuwaje?
AY: Ni jinsi labda vyombo vya habari huwa vinafanya au wenyewe tu kwa juhudi zao lakini wanamuziki wapo wengi wanaweza kufanya vizuri sana ni kuwapatia platifomu tu.
Spoti Xtra: Imekuwaje mpaka ukaamua kutoka Tanzania mpaka Rwanda?
AY:Mtu yeyote anafaa tu sionagi sababu ya kuangalia mipaka kwa sababu kwa sasa Dunia ya utandawazi,na watu wameingiliana sana, Tanzania yenyewe tu, wameingiliana makabila mbali mbali kwa hiyo sikuona sababu ya maana tukifikiria hivyo tutarudisha yake mambo ya kizamani kwamba lazima mtu uoe kabila lako,mapenzi hayahusiani na ukabila wala Utaifa.
Spoti Xtra: Mlikutana wapi kwa mara ya kwanza?
AY: Nilikutana naye Rwanda nilienda kutembea tu japokuwa familia zetu zilikuwa zinajuana.
Spoti Xtra:Tukio gani ambalo limekutokea katika maisha yako hautaweza kulisahau?
AY:Ni mama yangu alipofariki.
CHANZO: SPOTI XTRA
0 COMMENTS:
Post a Comment