July 16, 2019


MSIMU mpya wa 2019-20 utakuwa ni moto wa kuotea mbali kutokana na timu zote kujipanga vema msimu huu wa usajili ili kufikia malengo ambayo wameyapanga.

Mpaka sasa hekaheka za usajili zinaendelea huku kila timu ikitamba kufanya usajili kwa matakwa ya ripoti ya mwalimu na wana imani kubwa kwa wachezaji ambao wamesajiliwa.

Wengi wao waliopata ulaji, rekodi zinaonyesha kwamba walizisumbua Simba na Yanga na kwa sasa tayari wamepata ulaji kwenye timu nyingine kama ifuatavyo:

Kassim Khamis

Nyota huyu amesajiliwa na Azam FC kwa kandarasi ya miaka miwili ametoka Kagera Sugar inayoshikilia rekodi ya kuvuna pointi sita mbele ya Simba ya Mbelgiji Patrick Aussems msimu wa 2018-19.

Kwenye mchezo wa kwanza walipokutana na Simba uwanja wa Kaitaba alifunga moja ya bao kwenye ushindi wa mabao 2-1 hali iliyompandisha chati na kuitwa ndani ya Azam FC, pia Simba na Yanga zilikuwa zinaiwainda saini yake.

Idd Suleiman

Mshambuliaji mpya wa Azam FC, amesaini kandarasi ya miaka miwili ametokea Mbeya City. Deogratius Munish ‘Dida’ anaijua shughuli yake kwani alimtungua bao moja msimu uliopita mchezo ulichezwa uwanja wa Sokoine licha ya Simba kushinda mabao 2-1.

Ramadhan Kapela

Mshambuliaji huyu nyota yake iling’ara kwenye mchezo wao dhidi ya Simba alipokuwa Kagera Sugar ambapo alihusika kwenye mabao yote mawili, kwa kutoa pasi ya bao kisha naye akafunga bao lililoipa Kagera Sugar pointi tatu uwanja wa Kaitaba mbele ya Simba.

Kwa sasa ujuzi wake utaonekana na watoto wa mjini Kino boys kwa kuwa amesaini kandarasi ya miaka miwili.

Jacob Massawe

Alikuwa nahodha wa Stand United mchezo wa kwanza wa Yanga kupoteza ilikuwa uwanja wa Kambarage ambapo Jacob Massawe alifunga bao hilo dakika ya 88, kwa sasa amejiunga na Gwambina FC kwa kandarasi ya mwaka mmoja na timu yake ya Stand United nayo ilishuka daraja.

Salim Aiyee

Alikuwa na msimu mzuri kwa mwaka 2018-19 aliifunga Yanga nje ndani kwani mchezo wa kwanza uliochezwa uwanja wa Mwadui Complex licha ya Yanga kushinda mabao 2-1 na ule wa marudiano uliochezwa uwanja wa Taifa alifunga bao licha ya Yanga kushinda mabao 3-1.

Kwa sasa amesaini kandarasi ya miaka miwili ndani ya KMC, alimaliza msimu akiwa amefunga jumla ya mabao 18 dili lake la kutimkia Swedeni ilibuma kwa kukosa viza.

Vitalis Mayanga

Alizua gumzo kwa kuwapiga chenga magolikipa wawili wa Yanga ambapo alianza na Beno Kakolanya ambaye yupo Simba kwa sasa, kwenye mchezo uliochezwa uwanja wa Taifa kabla ya kutoa pasi ya bao na akamalizia na mlinda mlango Klaus Kindoki uwanja wa Nangwanda na alifunga bao.

Kwa sasa ni mali ya KMC alimaliza msimu akiwa na mabao 10, alisajiliwa kimkakati na Simba usajili wa awali kabla ya mkataba wake kuvunjwa.

Ally Ally

Beki mpya wa Yanga wengi wanapenda kumwita ‘Mwarabu’ amesaini kandarasi ya miaka miwili ndani ya Yanga, licha ya kujifunga bao 1 alipokuwa anaitumikia KMC ilipocheza dhidi ya Yanga uwanja wa Taifa bado uwezo wake ulikuwa ni tishio kwa wapinzani.

Simba na Yanga hawakuwa na raha anapokuwa uwanjani kwani alikuwa ni mtibua mipango kwa hatari nyingi ndani ya uwanja, kwa sasa ni mali ya Yanga.

Raizin Hafidh

Kasi yake akiwa uwanjani na uwezo wa kujiamini viliipa taabu safu ya ulinzi ya Simba na aliwafunga nje ndani kila walipokutana kwa kuanza mchezo wa kwanza uwanja wa Mkwakwani ambapo Simba ilishinda kwa mabao 2-1 na ule uliochezwa uwanja wa Taifa ambapo Simba iliibuka na ushindi wa mabao 8-1.

Kwa sasa amepewa kandarasi ya mwaka mmoja ili kuongeza nguvu kwenye kikosi cha Gwambina FC ambacho kinashiriki Ligi Daraja la Kwanza.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic