August 1, 2020



KESHO Jumapili, tunatarajia kushuhudia mchezo wa mwisho kwa msimu huu wa soka wa 2019/20 Tanzania Bara. Kumbuka msimu huu ulianza Agosti, 2019.

Mchezo huo wa kufunga msimu huu utakuwa ni wa fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam maarufu Kombe la FA utakaozikutanisha Namungo FC dhidi ya Simba SC.

Katika Uwanja wa Nelson Mandela kule Sumbawanga mkoani Rukwa, ndipo mchezo huo utachezwa na kumpata bingwa mpya wa michuano hiyo.

Kila upande umekuwa ukijinasibu kuibuka na ushindi, Simba wamepania kushinda huku wakitaka kuchukua taji la tatu msimu huu, Namungo wao wanataka kuchukua taji hilo na kuweka heshima.

Namungo msimu huu kwao ni wa kwanza kucheza Ligi Kuu Bara, wamefanya vizuri katika ligi na kumaliza nafasi ya nne ikiwa na pointi 64. Simba ni mabingwa wakikusanya pointi 88. Timu zote zilicheza mechi 38.

Katika ligi, timu hizo zimekutana mara mbili, Simba imeibuka wababe kwa kushinda mechi moja na sare moja, hivyo Namungo wana muda wa kujiuliza hapo kesho.

Binafsi nautazama mchezo huu kama mmoja kati ya mchezo ambao utakuwa wa kuvutia sana kutokana na timu zinazokwenda kukutana hapo kesho.

Kitendo cha Namungo kupanda daraja, kisha kumaliza ndani ya nne bora kwenye ligi si cha kubeza. Hii inanikumbusha KMC ya msimu wa 2018/19 ambayo ilikwenda kushiriki Kombe la Shirikisho Afrika.


Namungo wanaonekana kujipanga kufanya kweli, katika hilo wameanza kufanikiwa kwenye ligi, kazi iliyobaki sasa ni katika mchezo huo wa kesho kuona wanamaliza kazi.

Kocha wao, Hitimana Thiery, amewazungumzia Simba akisema licha ya kwamba ni mabingwa wa ligi, haimaanishi wao wataingia kinyonge, wanawaheshimu kwanza, lakini mambo mengine yatafuata.

Simba nao kupitia kwa kocha wao, Sven Vandenbroeck, amesema anawaheshimu Namungo na anaona mchezo utakuwa mgumu, lakini wanajipanga kushinda.

Kila mmoja anataka kushinda, hapo ndipo utaona namna gani mchezo huu utakuwa mgumu, lakini angalizo ni kwamba, waamuzi waliopewa dhamana ya kusimamia mchezo huu, wazitafsiri vema sheria 17 za soka.

Tunataka kuona mchezo wa haki, hatutaki kusikia baada ya mchezo kwamba kuna timu imependelewa, hiyo haitaleta picha nzuri kabisa.

Atakayeshinda ashinde kwa uwezo wake au kwa bahati kwa sababu tunatambua kwamba kwenye soka kuna ishu ya bahati au uwezo.

Timu inaweza kuwa na uwezo mkubwa, lakini ikakosa bahati, ikapoteza mchezo, lakini wakati mwingine timu inakuwa na hivyo vyote, hapo inakuwa rahisi kuibuka na ushindi tena mnono.

Ikiwa ni mchezo wa mwisho wa kufunga msimu huu, tunataka kuona kila upande ukionesha ujuzi wake ule ambao kila mmoja ataufurahia kwa maana ya mashabiki na watazamaji kwa jumla.

Wale watakaokuwa uwanjani na watakaoshuhudia mchezo kupitia runinga, wanataka kuona soka la ufundi na sio butuabutua.

Wachezaji kumbukeni kipindi kijacho ni cha usajili, mnaweza kuutumia vema mchezo huu kujiuza, hivyo nafasi hii itumieni vema.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic