September 3, 2020

 



NA SALEH ALLY

UKIANGALIA takribani wiki mbili, Yanga wamekuwa wakipambana kuhakikisha wanafanya kitu kizuri katika tamasha lao.


Jana ndio ilikuwa ni hatma ya Wiki ya Mwananchi, tamasha ambalo limefanyika kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.


Yanga ilikuwa ni lazima wapambane kuhakikisha tamasha lao linakuwa kubwa na kufanikiwa ili kuonyesha misuli dhidi ya watani wao wa jadi Simba.

Simba walifanya tamasha lao maarufu la Simba Day na kuonyesha kwamba isingekuwa kazi nyepesi kwa Yanga kujitokeza kwa wingi kiasi chao.


Hata hivyo, Yanga wameonyesha ni wakubwa, wana watu na inawezekana kuujaza uwanja kamna ambavyo wamefanya. Pamoja na kwamba kumekuwa na ule utani kutoka kwa Msemaji wa Simba, Haji Manara kwamba kiwango cha kiingilio kuwa kidogo, ndicho kilichowabeba Yanga lakini bado hii haifuti ile maana kwamba kweli wana watu na wanakubali.


Kwa watu 60,000 haiwezi kuwa shida kwa Simba au Yanga kulingana na ukubwa au ukongwe wa klabu hizi kwa kuwa tunafahamu bila ya ubishi kwa kila moja kuwa na mashabiki zaidi ya milioni 15, wala si jambo la kushangaza.


Hivyo ni namna tu ufanyeje ili mashabiki hao waweze kukusanyika pamoja. Wote wameshaonyeshana nguvu, kila mmoja kupitia hilo atamuonyesha mwenzake kuwa yuko vizuri lakini ninaona ni vizuri kuwakumbusha Yanga kuwa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2020-21, inaanza baada ya wiki moja.


Kinachofuatia sasa maana yake ni kuwekeza nguvu nyingi katika hatua inayofuatia ambayo ndio yenye majibu mengi kwa kila kilichokuwa kikiandaliwa.


Mara nyingi sana, kumekuwa na hali ya mshituko kwa timu hizi kongwe baada ya matamasha haya kwa kuwa huenda wanatengeneza matumaini makubwa kuliko hali halisi.


Matumaini yanaweza kuwa makubwa kwa kuwa katika siku zao maalum kama tamasha la jana, kunakuwa hakuna mechi ya mashindano. Wanakuwa na mechi maalum ya kujifurahisha ambayo haina presha kubwa na kila kitu kinaonekana ni kikubwa na kinawezekana.


Mashabiki wanaondoka uwanjani wakiwa na matumaini makubwa. Ajabu, ligi ikianza, mara timu imepoteza dhidi ya Kagera Sugar na kadhalika, jambo ambalo linawachanganya sana mashabiki kwa kuwa wanakuwa hawakutarajia kabisa.


Timu nyingi za Ligi Kuu Bara kwa sasa ziko katika maandalizi tena kimyakimya. Yanga wanakuwa na mambo mengi ya kufanya kutokana na ukongwe au ukubwa wa klabu yao. Kwa sasa, hauwezi kusema wameelekeza hasa nguvu katika kikosi chao.

Nasema hivyo kwa kuwa kocha mkuu, ndio amewasili siku chache na yeye anakiona kikosi chake akiwa mgeni. Hivyo anahitaji muda wa kutosha kuwa na timu yake na sote tunakubali, wiki moja, haiwezi kuwa inatosha kwa kiasi cha uhakika.


Wachezaji wengi wa Yanga ni wageni, maana wameachwa zaidi ya wachezaji 14, wamesajiliwa zaidi ya 10, hili haliwezi kuwa jambo jepesi katika kikosi.


Inawezekana linachukuliwa kawaida sana, lakini bila ya ubishi, Yanga wanahitaji muda bora wa mazoezi na kuunganisha kikosi chao na picha ya ubora wa uhakika haiwezi kuwa kupitia kilele cha Wiki ya Mwananchi.


Lazima Yanga itulie na kuamini inatakiwa kuunganisha vipande vya kikosi chao ili kujenga timu bora kabisa ambayo wameisajili na kwa kuwa muda ni mchache, lazima masikio na macho yawekezwe katika kikosi kwa ajili ya kukijenga na kukipanga upya.


Yanga wasibeze hili kwa kuwa tayari wametengeneza presha ya Imani, kwamba wana wachezaji wazuri lakini kumbuka, hata uwe na wachezaji wazuri vipi, kama mfumo wa kuwaunganisha ni duni, basi tegemea majibu ya kushitukiza. 


2 COMMENTS:

  1. Saleh Ali mbona hukuwapa wosia simba baada ya simba day?mnazi mkubwa tukutane October 18 baada ya huu wosia

    ReplyDelete
  2. hujakosea sema umezid kwa yanga kumbuka simba azam nao walikuwa na matamasha mbona hujaongea

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic