November 16, 2020


 


TANGA imekuwa maarufu katika mchezo wa ngumi za kulipwa kupitia Hassan Mwakinyo kutokana na rekodi anazoendelea kuweka katika mchezo huo.


 Lakini wapo mabondia wengi wakali wanajua kazi yao ndani ya ulingo isipokuwa hawajatoka tu, sasa huyu ni Adam Yusuph Chiga mmoja kati ya mabondia matata sana wanaotokea Makorora jijini Tanga.


 Kijana mmoja mpole sana lakini anaposimama ndani ya ulingo anakuwa na roho ya kinyama kutokana na kushusha vyuma vya maana kwa wapinzani wake.


Chiga anatarajia kupanda ulingoni Novemba 28, mwaka huu kuzichapa dhidi ya Adam Kipenga katika pambano litakalofanyika kwenye Ukumbi wa Next Door Masaki jijini Dar chini ya udhamini wa Gazeti la Spoti Xtra, +255 Global Radio, DSTV, Plus TV,  Clouds Media, Precision Air, Smart Gin, Kebbys Hotel na Uhuru FM.


Championi limefanikiwa kufika jijini Tanga na kumshuhudia bondia huyo akiendelea na maandalizi ya pambano lake hilo chini ya kocha wake Zuber Abdulrahman ‘Mabele’ pamoja na kuendelea na shughuli zake za bodaboda.

 

Chiga anasema kuwa: “Mimi ni mtoto wa tatu katika familia ya watoto watatu ambao kuna wanawake wawili na wakiume mmoja ambaye ndiyo mimi Adam.


“Katika familia yetu peke yangu ndiyo nacheza ngumi yaani bondia lakini dada zangu wao wanaendelea na shughuli zao nyengine.


“Naamini ngumi zitanifikisha mbali kwa sababu nina kipaji cha mchezo huu halafu pia naupenda lakini bado napata sapoti ya kutosha kutoka kwa watu wangu hasa wa mtaa wa Kwa Njeka ambao natokea pia maskani zangu za  Jerry Press na  Johannesburg.


“Binafsi nimejiandaa vizuri kwa sababu hakuna pambano dogo maana hata mpinzani wangu naye amejiandaa hivyo sitegemei kuona pambano rahisi isipokuwa malengo yangu ni kupata ushindi hilo ndiyo kubwa.


“Mbali ya ubondia nafanya kazi ya kusafirisha watu kwa kutumia pikipiki yaani Bodaboda ndiyo kazi kubwa ambayo naitegemea kuendeleza maisha.

 

 “Unajua ngumi hatupigani kila siku ndiyo maana nafanya kazi hiyo na ratiba yangu inaenda sawa kila siku kwa kuwa usaidizi wa kutosha kutoka kwa watu wananiunga mkono.


 “Nategemea ushindi katika pambano langu hilo ndiyo jambo kubwa kwa sasa, nashukuru familia yangu nayo inaniunga mkono kwa asilimia zote hivyo sitaki niwaangushe pale Next Door Masaki,” anasema  Chiga.

Mama yake afunguka

Championi halikuishia hapo kwani lilifanikiwa kuzungumza na  mama mzazi wa bondia huyo, Saum Ramadhani ambaye kwa upande wake amesema alivyogundua kipaji cha mtoto wake katika suala zima la mchezo wa ngumi.


“Niligundua kipaji chake wakati anaanza lakini hata ilipokuwa ikitokea amefanya kosa basi ukitaka kumuadhibu ilikuwa shughuli pevu kwa sababu alikuwa na nguvu za mikono.


 “Kiukweli hapo ndiyo nikajua kwamba anakipaji na alipomaliza elimu yake ya sekondari ndiyo akaingia rasmi kwenye mchezo huu wa ngumi.


“Nilichokifanya nikumuunga mkono na kumwambia aongeze bidii katika mazoezi yake kwa sababu michezo sasa hivi ni ajira lakini pia wazazi wengine wawaunge mkono vijana wao waliojiingiza kwenye michezo.


“Kitu kikubwa ni kumuombea afanye vizuri katika pambano lake la Novemba 28, matumaini yangu kwamba siku hiyo nitakuwepo kumuunga mkono,” anasema  Saum.

Wengine watakaopanda ulingoni ni Idd Pilali dhidi ya Arnel Tinampay kutoka Ufilipino, Salim Mtango na Eduardo Mancito wa Ufilipino, Adam Yusuph dhidi ya Adam Kipenga.


 Wakati Seleman Kidunda atazichapa na Said Mbelwa, Ismail Gali ya tano dhidi ya Mustafa Dotto, Ramadhan Shauri vs Saleh Mkalekwa na Stumai Muki vs Lulu Kayage.


Pambano hilo ambalo litakuwa kwa kiingilio cha Sh 20,000 mzunguko, Sh 50,000 kawaida na Sh 100,000 kwa VIP.

 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic