April 15, 2021


HESABU ambazo zipo kwa sasa kwa kila timu ni kuona namna gani ambavyo zinaweza kuvuna pointi tatu kwenye mechi zao ambazo watacheza kwa sasa.

 Sio kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara pekee bali ni mpaka Ligi Daraja la Kwanza, Ligi Daraja la Pili hakuna timu ambayo inalala kwa sasa macho yote ni kwenye mechi zao zilizobaki.

 Hakuna tena neno la hii ni timu ndogo ama hii ni timu kubwa, zote zinakazana kusaka matokeo ili mwisho wa siku zipate ushindi.

 Itazame Mwadui FC ambayo inaburuza mkia ilipokutana na Azam FC, Uwanja wa Azam Complex ilikubali kupoteza ila ngoma ilipokwenda kupigwa pale Mwadui Complex, ubao ulisoma Mwadui 0-0 Azam FC, waligawana pointi mojamoja.


Hakuna unyonge kwa timu ambazo zinashuka uwanjani mzunguko huu wa pili, kila mtu anaonyesha uwezo wake wote kusaka pointi tatu.


KMC walipokutana na Yanga mzunguko wa kwanza ubao ulisoma KMC 1-2 Yanga na ngoma ilipokuja kuchezwa Uwanja wa Mkapa ilikuwa ni 1-1.

 

Licha ya kwamba wimbo mkubwa ambao unaimbwa na kila mmoja kwa upande wa wachezaji pamoja na viongozi ni kwamba waamuzi wamekuwa hawatabiriki, bado kupata matokeo ni kazi kwa wakati huu.

 

Hili ni jambo jema kwani ushindani unavyokuwa mkubwa ligi ya Tanzania inazidi kuwa imara na kufanya bingwa ajaye ajipongeze pale atakapotwaa taji lake.

 

Lakini kumekuwa na kasumba ya timu nyingi kuweka mtego kwamba mechi za mzunguko wa kwanza huwa wanazichukulia kawaida, hakuna yale mapambano ya kweli yanayoonekana.

 

Imekuwa kawaida kwamba pale wanapopoteza utasikia bado kuna mechi zinakuja mbele hivyo tuna nafasi ya kubaki ndani ya ligi.

 

Hizo mechi ambazo zinakuja zimekuwa zikiwapa presha na kufanya hata mpira wakitoa wao ukirushwa kwa timu pinzani wapeleke lawama kwa waamuzi wakidhani wanaonewa.

 

Sababu ya hayo kutokea ni ile presha ya mchezo, kila mmoja yupo kwenye presha, wachezaji, benchi la ufundi mpaka mashabiki nao wanasumbuliwa na presha ya kuona matokeo yanatokea hapohapo.

 

Hili linapaswa litazamwe kwa ukaribu na timu kiujumla ili kuweza kupunguza presha ambazo zinaweza kuzuilika mwanzo kabisa wa ligi kwa hesabu za kuamini kwamba kila mchezo ni muhimu.

 

Suala la kuamini kwamba kuna mechi mkononi ni ugonjwa ambao unahitaji tiba. Ili kuweza kupunguza presha ni kuamini kwamba mechi zote ni fainali na kucheza bila kukamia baadhi ya mechi.

 

Pia kwa wachezaji wakiwa uwanjani bado ninawakumbusha kwamba wasitumie presha yao kuwaumiza wachezaji wengine kwa makusudi hili hapana nasema tena hapana.

 

Kwa wale mashabiki wenye tabia za kutoa maneno yasiyo  mazuri kwa viongozi pamoja na wachezaji wanapaswa nao wawe na subira na kukubali matokeo ambayo wanayapata.

 

Imani yangu ni kwamba waamuzi watatembea na zile kanuni zao 17 katika majukumu yao huku wachezaji nao wakicheza , ‘fair play’.

 

Hii ni lala salama , wachezaji wanatengeneza ugali wao hivyo ukimtibulia mwenzako utakuwa unataka ashinde njaa, hilo halipendezi, chezeni mpira kwa juhudi ila faulo zile za kutengeneza acheni.

 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic