September 10, 2021


MLINDA mlango mpya wa Yanga, Erick Johora ameukubali mziki wa tizi linalotolewa na benchi la ufundi la klabu hiyo chini ya kocha mkuu Mtunisia, Nasreddine Nabi, na kuweka wazi kuwa wako tayari kupambana katika mchezo wao wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Rivers United ya Nigeria.

Johora ambaye ni raia wa Tanzania amejiunga na Yanga akitokea Aigle Noir ya Burundi aliyohudumu msimu uliopita, ambapo alitangazwa rasmi Agosti 10, mwaka huu na ni miongoni mwa nyota 11 wapya waliosajiliwa kwa ajili ya msimu ujao wa 2021/22.

Baada ya kuwa na maandalizi ya muda mrefu ya kabla ya msimu ‘Preseason’ Yanga Jumapili hii wanatarajia kuanza kibarua chake cha kwanza cha msimu wa 2021/22 katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Rivers United ya Nigeria, utakaopigwa kwenye Uwanja wa Mkapa kabla ya mchezo wa marudiano kupigwa Septemba 19, mwaka huu.

Akizungumzia maandalizi yao, Johora amesema: “Tumekuwa na maandalizi bora kuelekea mchezo wetu dhidi ya Rivers United, tuna nafasi kubwa ya kufanya vizuri hasa kutokana na programu ambazo benchi la ufundi chini ya kocha mkuu wamekuwa wakitupatia, lakini pia kwa kuwa tutakuwa Uwanja wa nyumbani.

“Ni kweli utakuwa mchezo mgumu kutokana na uhalisia kwamba ni mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika, lakini tutapambana kuhakikisha tunapata matokeo mazuri katika mchezo huo.”

 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic