Kocha Mkuu wa timu ya taifa ya Zanzibar,
Zanzibar Heroes, Salum Bausi, amemteua kiungo wa Azam FC, Hamis Mcha kuwa
nahodha wa kikosi hicho katika michuano ya Chalenji.
Michuano ya Chalenji inatarajiwa kuanza
kutimua vumbi keshokutwa jijini Nairobi, Kenya.
Mcha ameteuliwa kushika wadhifa huo
badala ya Nadir Haroub ‘Cannavaro’ ambaye ametemwa katika kikosi hicho.
Bausi
amesema ameamua kumpa kitambaa hicho Mcha kutokana na nidhamu kubwa ambayo
amekuwa akiionyesha tangu akiwa na klabu yake mpaka kwenye timu ya taifa.
“Ni kijana mwenye nidhamu ya hali juu,
iwe kwenye klabu yake ama hapa. Hakika ni mfano wa kuigwa kwa wachezaji
wengine. Nina imani naye kuweza kuongoza kundi la watu wazima kutokana na
nidhamu anayoionyesha kila siku,” alisema Bausi.
Cannavaro na Aggrey Morris walitemwa kwa
kile alichosema ni kutokana na utovu wa nidhamu wa kugawana fedha kiasi cha
dola 10,000 walizopata kama tuzo ya mshindi wa tatu kwenye michuano ya mwaka
jana nchini Uganda.
Bausi aliongeza kuwa, kikosi hicho
kinatarajia kuondoka leo Jumatatu kwenda Kenya ili kujiweka ‘fiti’ kabla ya
mchezo wa kukata utepe dhidi ya Sudan Kusini Jumatano.
0 COMMENTS:
Post a Comment