Kiungo nyota wa zamani wa Yanga, Athumani Iddi ‘Chuji’ ameibuka
na kuvunja ukimya kuhusiana na suala la timu gani ataichezea msimu ujao.
Dirisha la usajili wa Ligi Kuu Bara linafungwa leo saa 5:59.
Chuji amefanya mahojiano na SALEHJEMBE na kusema hana mpango wa
kusajili Mwadui FC ya Shinyanga kama ambavyo imekuwa ikielezwa.
MWadui FC inafundishwa na kocha wa zamani wa Simba, Jamhuri
Kihwelo ‘Julio’.
“Anayesema nimesajili Mwadui ni nani, mimi nasikia habari hizo
watu wanasema.
“Nilikuwa nafanya mazoezi na veterani, hata kama nilifanya na
Mwadui lakini sijazungumza na kiongozi yoyote wa Mwadui wala sina mpango wa
kusajili.
“Kwa kifupi sijasajili timu yoyote ya Tanzania, hivyo naomba
watu wasubiri,” alisema Chuji akijiamini.
Hata hivyo, blog hii ilishaandika taarifa za Chuji kutaka kwenda
kukipiga Uarabuni ambako amepata timu.
“Bado kuna mambo ninafanya, baada ya kukamilika nitaeleza, ndiyo
maana ninashangazwa na taarifa hizo za kuichezea Mwadui,” alisema kiungo huyo
ambaye msimu uliopita, Yanga iliamua kumuacha na kusababisha baadhi ya wajumbe
wa kamati ya usajili na ile ya mashindano ya Yanga, kugawanyika.
0 COMMENTS:
Post a Comment