December 3, 2014

EMERSON

Na Saleh Ally
YANGA imemleta kiungo Emerson Roque ambaye tulielezwa amekuja kwa ajili ya kufanya majaribio ya wiki moja hadi mbili.


Amefanya kwa siku tatu, benchi la ufundi la Yanga limetangaza kuridhishwa na kiwango chake na baada ya hapo amepewa mkataba wa mwaka mmoja.

Majaribio ya siku nne! Tena Yanga ikiwa inafanya mazoezi ya kukimbia, hajapewa hata mechi? Kwa maelezo ya mwanzo ya uongozi wa Yanga, kidogo inashangaza!

Lakini kwa maana ya hali halisi, uwezo wa kiungo yule kupitia video inayoonyesha mechi zake mbalimbali, anastahili kupewa mkataba. Lakini kwa nini sasa uongozi ulisema unamfanyia majaribio?

Simba nao wamemleta kijana Omar Mboob raia wa Gambia ambaye wengine walisema anatokea Gabon. Kijana huyo tayari yuko nchini, ameanza majaribio na Simba, wamesema atakuwa nchini kwa wiki mbili.

Hatujajua kama Simba nao watakwenda kwa njia ileile waliyopita Yanga, ya kusema anafanya majaribio halafu Mgambia huyo apewe mkataba ndani ya siku tano tu kwa madai benchi limeridhika wakati majaribio yalikuwa ni ya danadana bila hata mechi!
 
MBOOB
Lengo si kukosoa Simba au Yanga walivyofanya, kwanza ni kueleza kwamba walichokifanya si utaratibu mzuri wa kuwajaribu wachezaji. Vizuri zaidi, wangekaa kimya tu bila ya kutangaza ni majaribio.

Muhimu hasa ni suala la nini klabu zinaingiza, nini zinatoa hasa katika suala la gharama. Ndiyo maana naangalia kama kweli usajili wa wachezaji kutoka nje unakuwa ni muhimu au fasheni tu.

Yanga na Simba zimekuwa zikihaha kulazimika kuongeza fungu la fedha ili kukamilisha mishahara ya mwezi ya wachezaji. Bia ya Kilimanjaro ambayo ni mdhamini wao, inatoa kipande cha mshahara.

Mshahara wanaotoa Kilimanjaro, kama ungepelekwa Mtibwa Sugar, Kagera Sugar au timu nyingine ambayo si Yanga, Azam FC au Simba, ungetosha vizuri sana.

Msisitizo ni kwamba, mishahara kwa timu kongwe za Yanga na Simba, unakuwa juu sana kutokana na gharama ya juu wanaolipwa wageni kama akina Emerson na wenzake. Je, wana tofauti kubwa sana na wachezaji wa hapa nyumbani?

Wakati Simba na Yanga zinagharimia wageni kwa kiasi kikubwa, zinajua kwamba zinacheza na hasara bila ya sababu za msingi.

Mfano, Simba inaonekana isingehitaji kuongeza mchezaji wa kigeni katika kipindi hiki ili kubana matumizi kwa kuwa haina michuano ya kimataifa na kuna uwezekano wa kupata kiungo bora hapa nyumbani kama kutakuwa na uchambuzi wa kutosha kutafuta kiungo bora.

Mimi ninaona Yanga na Simba zinapata hasara kubwa kutokana na gharama za matumizi ukilinganisha na kipato chao kwa wakati huu. Sababu hizi hapa.



Mechi:
Mechi za ligi ni nne tu kwa mwezi, moja kwa kila wiki. Maana yake wachezaji wanaweza kuitumikia timu na kuingiza fedha kwenye klabu mara nne tu kwa mwezi.

Hii inatokana na ratiba ya ligi kuwa kila timu inacheza mara moja kwa wiki.

Hakuna anayeweza kukataa kuwa soka ni biashara, timu inatakiwa kushinda ili kuongeza imani kwa mashabiki wake ili wajitokeze kwa wingi uwanjani. Lakini inaposhinda na kufanikiwa kubeba kombe au nafasi ya pili, inashiriki michuano ya kimataifa na kuingiza fedha zaidi kama itafanya vizuri.

Kwa misimu miwili, Simba imekuwa na wachezaji wa kimataifa, haikushika hata nafasi ya pili. Hii inaonyesha kuna tatizo, pia inathibitisha wachezaji wa nyumbani wakipewa nafasi, wnaweza wakafanya vizuri na kusaidia kupunguza gharama kama zile za kuwasafirisha wachezaji wa nje, kulipia vibali vya kufanya kazi nchini na kadhalika.

Azam TV:
Kuonyeshwa moja kwa moja kwa mechi kupitia Azam TV, bado ni tatizo kwa timu hizo mbili kubwa, kwani watazamaji wanapungua kwa wingi viwanjani.

Sh milioni 100 inayotolewa na Azam TV kwa msimu, bado haitoshi kwa Yanga na Simba ambazo zinaweza zikaingiza fedha kama hizo katika mechi moja tu.

Hakuna ubishi kama ambavyo Yanga walikuwa wakidai, timu hizo mbili ndizo zinazovuta watu wengi zaidi. Kweli zilistahili kulipwa zaidi ya nyingine na ilikuwa ni haki, lakini kwa fedha zinazopata sasa, si sahihi.

Suluhisho:
Kupunguza ukubwa wa hasara kila kukicha, Yanga na Simba zinapaswa kuangalia suala la kutumia wachezaji wengi zaidi wa nyumbani,
kwani wachezaji wengi wanaoletwa wanakuwa hawana viwango tofauti sana na wale wa hapa nyumbani.

Bado naendelea kupinga kusema Hamisi Kiiza wa Yanga, ana tofauti kubwa na Mussa Hassan Mgosi ambaye anamzidi umri.

Iwapo timu hizo zitaendelea kukubali kuangalia ushabiki, kujaza wachezaji wa kigeni rundo huku zikiendelea kulimbikiza madeni kutoka kwa wadau au wanachama wake, haitakuwa sahihi.

Deni kila linavyozidi kupanda, huongeza presha au kuvuruga uhusiano kati ya pande mbili zilizokubaliana. Kwa urahisi zaidi, iko haja ya kuwa na timu imara na makini za kusaka, kufufua na kuviendeleza vipaji hapahapa nyumbani, inawezekana kabisa.



1 COMMENTS:

  1. Huwa nashindwa kuelewa mada zenu, kwa miaka ya karibuni ni mchezaji gani wa Tanzania ambaye amekuwa mfungaji bora angalau kwa miaka miwili mfululizo!? Unamzungumzia Mgosi, hivi kwanini kama yeye ni bora hayuko Azam, Yanga wala Simba!? Tatizo la wachezaji wa kibongo hawajitambui na hawana malengo. Mtu kama Samata na Ulimwengu ni mfano wa kuigwa Tanzania. Muangalie leo chuji, kila siku anajisifia hakuna midle kama yeye bongo na mimi nakubali, lakini hajitambui sasa wanini kwenye club!? huwezi kulinganisha Simba/Yanga/Azam na Mtibwa, wakati mtibwa anacheza ili ashike nafasi za juuu wenzake wanaangalia ubingwa na mechi za kimataifa.

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic