May 29, 2015


Na Saleh Ally
KAMA utakuwa mfuatiliaji wa mambo, hakika utakuwa umeona kazi safi na ya kuvutia ya mshambuliaji Carlos Arturo Bacca Ahumada anayekipiga katika kikosi cha Sevilla.


Sevilla sasa ndiyo mabingwa wa Ligi ya Europa kwa miaka miwili mfululizo, lakini wakiweka rekodi ya kubeba kombe hilo mara nne katika miaka tisa.

Katika kuutwaa ubingwa huo mara mbili mfululizo, huwezi ukatoa pongezi bila kumzungumzia mshambuliaji huyo hatari mwenye sura kama vile hawezi kabisa kucheza soka.


Bacca ndiye amekuwa chachu ya mabadiliko makubwa ya ukali wa safu ya ushambuliaji ya Sevilla ambayo imemaliza La Liga ikiwa katika nafasi ya tano baada ya mabingwa Barcelona, Madrid katika nafasi ya pili, pia Atletico Madrid na Valencia.

Kwa ufungaji mabao akiwa na 20, Bacca pia yumo katika tano bora baada ya kinara Cristiano Ronaldo (48), Lionel Messi (43), Antoine Griezman (22) na Neymar (22).


Asili ya Bacca ni nchini Colombia, mchezaji ambaye alianza kusaka maisha yake akiwa konda wa daladala katika mji aliozaliwa wa Puerto Colombia nchini Colombia.

Bacca, 28, aliishi maisha ya shida sana huku mpira ukiwa ni sehemu ya maisha yake lakini alishindwa kushiriki vya kutosha kutokana na ugumu wa kazi yake ya ukondakta aliyokuwa akiifanya.

Wakala mmoja ndiye aliyempeleka katika kikosi cha Atletico Junior huku akimuahidi atakuwa akimlipa fedha alizokuwa akipata kutokana na ukondakta. Alifanya hivyo baada ya kuona uwezo wake mkubwa wa kufunga mabao.


Bacca anaaminika ni mmoja wa wachezaji watano wabunifu zaidi duniani akiungana na Eden Hazard, Messi, Neymar na Ronaldo katika kundi la wachezaji wenye uwezo mkubwa wa kufunga na kutengeneza mabao.

Raia huyo wa Colombia aliishi maisha magumu sana, taarifa zinaeleza hata kupata mpenzi ilikuwa kazi kubwa kutokana na muonekano wake kama mtu mzima licha ya kwamba alikuwa na umri mdogo.

Karibu kila timu aliyoichezea katika maisha yake, ameibuka kuwa mfungaji bora wa kikosi hicho. Alitua barani Ulaya kwa mara ya kwanza mwaka 2012 na kuichezea St Bruges ya Ubelgiji ambako aliibuka mfungaji bora na mwaka uliofuata akajiunga na Sevilla.

Sevilla ambayo ilimsajili kwa euro milioni 7, imefaidika kwa kiasi kikubwa na mshambuliaji huyo asiyependa makuu na mjanja kweli akiziona nyavu mbele yake.
Kwa sasa ndiye anayepewa nafasi ya kuchukua mikoba ya Radamel Falcao katika kikosi cha Colombia na inaonekana yu tayari baada ya kuwa na mchezo mzuri katika mechi ya Kombe la Dunia dhidi ya Brazil nchini Brazil.

Konda huyo wa zamani nchini Colombia, sasa ndiye staa wa nchi hiyo na tabia yake ya utaratibu imemfanya awe kivutio zaidi kwa mashabiki wengi wa soka wa nchi hiyo.
Huenda kwa kuwa hajacheza Madrid au Barcelona, kumekuwa na ugumu kidogo kumsikia kila mara. Bacca ni mmoja wa washambuliaji hatari kabisa katika soka duniani.

Gazeti namba moja la michezo Hispania la Marca, lilimpa tuzo ya usajili bora wa msimu wa 2013-14 baada ya mafanikio makubwa ukiwa ni msimu wake wa kwanza Hispania.
Pia akabeba Tuzo ya Mchezaji Bora wa Amerika Kusini kati ya wale wanaocheza La Liga akiwapiga kumbo Angel Di Maria aliyeshika nafasi ya pili na Neymar aliyeshika namba tatu.

Kama ukipata nafasi mara nyingine, mfuatilie, huyu jamaa ni mbayaaa. Ana uwezo mkubwa sana wa kufunga, si muoga wa mabeki wakatili kama Pepe au Sergio Ramos na wengine wenye sifa hizo.

Amekuwa na ndoto ya kuifunga kila timu bora kwa sababu anaamini kila mshambuliaji bora, lazima aishinde safu bora ya ulinzi.

Bacca ambaye alikuwa mchezaji bora wa mechi ya fainali ya Europa walipocheza na Dnipro, juzi, ni mfano wa kuigwa, pia ni mchezaji ambaye Watanzania wanaweza kujifunza mengi huenda kuliko kwa Messi na Ronaldo.

Mtu huyu ni mchezaji aliyekubali kutimiza ndoto zake katika kipindi kigumu, kweli ameweza na umri unakwenda lakini uwezo wake, haujawahi kuyumba.






0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic