May 29, 2015


NINAAMINI utakuwa umesikia malalamiko ya wagonjwa ambao wamekuwa wakilalama kwamba baadhi ya wauguzi wa hospitali za serikali wamekuwa wakiuza dawa wodini.


Wauguzi hao ambao ni watu muhimu sana katika taifa letu, wameamua kuwa wachuuzi wa dawa kwa wagonjwa ambao baada ya kuandikiwa dawa, huambiwa hospitali haina dawa.

Baada ya muda, wauguzi hao hupita wakiuza dawa na hapo ndiyo maswali yanaibuka. Kwamba wanazitoa wapi wakati hospitali imesema imemaliza dawa. Swali au ndiyo zile zilizotolewa na serikali, halafu zimefichwa na sasa wagonjwa wanauziwa?


Swali jingine ni hivi, kama wauguzi ndiyo wanaouza dawa, unafikiri wanashindwa kushirikiana na madaktari wawaandikie wagonjwa rundo la dawa ili wauguzi hao wafanye biashara yao kwa faida kubwa?

Hakika hali hii inaonyesha kiasi gani watu tunaopaswa kuwaamini wanavyopotoka na kutuingiza hatarini na hofu kubwa ya maisha yetu hasa kwa wananchi wengi wa Tanzania wasiokuwa na uwezo, si sahihi.

Wakati tunaona wao wanafanya lisilo sahihi, najaribu kujiuliza maswali mengi kuhusiana na viongozi wengi wa soka ambao kama ilivyo kwa wauguzi, wanavyoweka rehani uhai wa soka la Tanzania ambalo hakika limekuwa likiendelea kupapasa huku wengi wakitaka lisifiwe kuwa linapiga hatua.

Kila mmoja anaweza kujisifia kwamba Tanzania inafanya vizuri kupitia klabu, mfano Yanga au Azam zilizoshiriki michuano ya kimataifa. Jibu litakuwa ziliishia palepale tulipozoea, kuwa “zilijitahidi”.

Nembo yetu ni kujitahidi. Mwisho wa hilo utakuwa lini? Hakika ni lazima hadi watu wakubali kubadilika kwenda katika njia iliyo sahihi na lazima viongozi wakubali kuwa watu wenye fikra endelevu na wakubali kupambana kweli. Ukisema nichague akili sahihi katika soka la Tanzania, basi nitachagua za mshambuliaji wa Tanzania, Mbwana Samatta.

Miaka mitano iliyopita, Samatta alikuwa tishio katika kikosi cha Mbagala Market iliyokuwa inashiriki Ligi Daraja la Kwanza Tanzania. Akacheza Simba nusu msimu tu, lakini sasa ana mambo mengi sana naweza kumfananisha na wenyeviti wa klabu kubwa za Yanga na Simba, matajiri wakubwa wa Tanzania.

Angalau ukisema gari, Samatta anatumia Range Rover Vogue ambayo hata kama thamani haitakuwa sawa na ile ya Yusuf Manji, Zacharia Hans Poppe na vigogo wengine wanaojulikana katika soka, lakini hatuwezi kukwepa kuwa ile ni Range Rover.

Tena ana vitu rundo, naweza kuonyesha anawazidi wachezaji wakongwe wenye majina makubwa kwa zaidi ya miaka kumi sasa. Unawajua, fungua tu macho utawaona.

Umaarufu wa Samatta kwa sasa unazidi ule wa mwenyekiti wa zamani wa Simba, Ismail Aden Rage, wenyeviti waliopita wa Yanga kama Francis Kifukwe na wenzake, Mwenyekiti wa zamani wa Fat, hata Rais wa sasa wa TFF, Jamal Malinzi.

Umaarufu huo wa Samatta umepaa ndani ya miaka mitano, tena baada ya kucheza miezi michache tu Ligi Kuu Bara ambayo wachezaji wengi wanaona ndiyo ndoto yao kuu.

Akaondoka kwenda DR Congo kujiunga na TP Mazembe huku wengi wakiamini ni nadra, atakwama na kurudi kama ambavyo wengine walivyoamua kurudi nyumbani akina Haruna Moshi ‘Boban’, Jerry Tegete, Shabani Kisiga na wengine wengi.

Kama utani, kinda huyo amekwenda akapasua anga hadi sasa amekuwa mfano wa kuigwa kila sehemu. Ndiyo maana nasisitiza kuwa nikiambiwa kuchagua, basi nitachagua akili yake ambayo ndani imejaa ujasiri unaowashinda Watanzania wengi.

Ubinafsi, kutaka kupata pekee, kutaka kushiba mwenyewe, kutamani kupaa kwa kujulikana sana, ndiyo imekuwa sehemu ya tatizo kubwa ya maendeleo ya soka la Tanzania ambalo kamwe siamini kuliita soka letu kutokana na udogo wake wa milele.


Sasa inaonekana tunahitaji akili za Samatta kwa wauguzi ili wasiuze dawa wodini na kuamini wanahitajika kuwasaidia Watanzania. Pia tunahitaji akili za kijana huyo wa miaka 23, kuzipandikiza kwa viongozi wa klabu, vyama na hata shirikisho ili mpira uende. Sijui hata kama zitatosha, aahh!

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic