November 9, 2015


Na Saleh Ally, Johannesburg
KIKOSI cha timu ya taifa ya soka ya Tanzania, Taifa Stars, kimeweka kambi jijini Johannesburg, Afrika Kusini kujiandaa na mechi dhidi ya Algeria.

Stars itaivaa Algeria katika mechi ya kuwania kucheza Kombe la Dunia mwaka 2018. Mechi hiyo itapigwa Novemba 14 jijini Dar es Salaam, kabla ya kurudiana Novemba 17 jijini Algiers.
Katika kambi ya Stars mjini hapa, karibu kila kitu kimekuwa kikionekana kwenda vizuri na matumaini ni makubwa kuwa Stars itafanya vizuri licha ya ubora wa Algeria.

 Bado inaonekana kuna mgawanyiko kati ya wapenda soka wengi. Wapo wanaoamini Algeria hawawezekani, lakini wapo wanaoamini kujituma, kufanya kazi ya ziada, inawezekana kabisa Stars ikawashangaza wengi.

Katika mahojiano na kocha wa Taifa Stars mzawa, Charles Boniface Mkwasa kuhusiana na hali ya kambi yake na muendelezo wa mipango.

Kambi hiyo iliyo katika Hoteli ya Holiday Inn Express ipo katika ulinzi mkali na utulivu wa hali ya juu.
Pia kambi hiyo imeandaliwa mpishi maalum ili kuhakikisha chakula cha wachezaji kinakuwa salama na wanakula wanachokihitaji.

SALEHJEMBE: Tuanze moja kwa moja, unaizungumziaje hii kambi ya jijini Johannesburg?
Mkwasa: Kwa ujumla kambi iko vizuri, iko katika sehemu nzuri na salama. Tunaamini malengo ambayo tulikuwa tumeweka basi tutayafikia.


SALEHJEMBE:Mazoezi ambayo umekuwa ukifanya yanaonekana ni makali sana. Unaweza ukazungumzia kwa maana ya kufafanua, hii maana yake nini?
Mkwasa: Wachezaji wametokea katika timu tofauti, tumeanza kutafuta ‘fitnesi’ ya pamoja. Mazoezi ni magumu sana lakini vijana wanaonyesha kujituma na huu ndiyo wakati mwafaka kufanya hivyo, kadiri siku za mechi zinavyosogea, hauwezi kufanya hivyo.

SALEHJEMBE: Lakini wachezaji hao wanatokea katika klabu zao walipokuwa wanacheza ligi. Kuna haja ya kuwafua kwa nguvu hivyo?
Mkwasa: Ni kweli wametokea kwenye ligi, lakini tumekuwa tukiwafuatilia kwa karibu na kuona fitnesi yao inapishana, ndiyo maana tumeamua kutafuta ya pamoja.

SALEHJEMBE: Algeria ina wachezaji wenye maumbo makubwa, warefu na wanatumia sana mipira ya juu. Mmejiandaa vipi kupambana na hilo?
Mkwasa: Mpira kawaida una mipango yake, bahati mbaya wachezaji wetu wengi wana maumbo madogo. Lakini hauchezwi kwa urefu. Utaona kuna timu zina wachezaji wafupi, mfano wa Lionel Messi lakini bado zimefanikiwa.
Kumbuka Hispania, Brazil walikuwa wana wachezaji wengi wafupi na wakabeba Kombe la Dunia.
Kikubwa tutajipanga kudhibiti mapema ujio wa mipira ya juu. Vizuri tahadhari kabla ya hatari.


SALEHJEMBE:Taifa Stars inaanzia nyumbani, mmejipanga vipi?
Mkwasa:  Hakika mpira wa sasa hauna nyumbani na ugenini. Lakini tumejipanga, tunajua tunatakiwa kuwa na matokeo mazuri yatakayotulinda mechi ya ugenini.

SALEHJEMBE: Mechi dhidi ya Nigeria, pia Malawi kikosi chako kilionekana kina makosa ya umaliziaji. Hili limefanyiwa kazi kweli?
Mkwasa: Kuna matatizo hauwezi kuyamaliza kwa siku mbili tatu. Tunaendelea kutengeneza kila mara tunapokuwa kambini ingawa umakini ungeweza kujengwa zaidi katika klabu zao kwa kuwa sisi tunakaa na wachezaji kwa muda mfupi sana.
Lakini hatuchoki, tunalifanyia kazi kila mara (suala la umaliziaji) kuhakikisha mambo yanakwenda sahihi. Tunaendelea kulikemea, ila halitaisha kwa siku moja tu.

SALEHJEMBE: Kuna mashabiki hadi sasa wanaamini Tanzania kuifunga Algeria, au kuing’oa ni ndoto. Hili linakuvunja moyo?
Mkwasa:  Mpira umebadilika sana, haujali nyumbani au ugenini na wala hauendeshwi tena kwa historia. Tunawaheshimu sana Algeria kutokana na ubora wao. Lakini tunataka kucheza nao na kushinda.


SALEHJEMBE: Ndiyo timu bora kabisa kutoka Afrika. Hauoni ni timu hatari kwa kikosi chako?
Mkwasa: Kweli ni wazuri na bora, tunaheshimu uwezo wao lakini tunachotaka ni kufanya vema na kushinda na katika mpira kutokana na mabadiliko, inawezekana. Angalia Iceland imeifunga Uholanzi, kwa sasa mambo hayo ni ya kawaida.
Utaona mechi na Algeria, wako walioamini tutafungwa tatu au nne. Lakini tukaonekana ndiyo tulistahili kushinda, lakini hatukuwa makini.

SALEHJEMBE: Hamkuwa makini, unafikiri mechi ijayo umakini umeongezeka?
Mkwasa:  Kadiri tunavyojifunza, inawezekana kabisa. Wachezaji wasikilize na kuelewa mafunzo yetu, halafu wayafanyie kazi. Ninaamini itawezekana.

SALEHJEMBE:Ikitokea umewakosa Thomas Ulimwengu na Mbwana Samatta. Unaamini kikosi ulichonacho hapa Johannesburg, kinaweza kupambana na Algeria na kushinda?
Mkwasa: Siwezi kufananisha ujuzi wa kila mmoja binafsi, pia siombi wasiumie. Lakini katika mpira lolote linawezekana. Tumewachagua vijana tuko nao hapa, ni bora na wanaweza kucheza ingawa watakosa uzoefu ambao wanao kina Samatta na Ulimwengu na kweli tunauhitaji sana uzoefu wao. Kwa vijana kupangwa dhidi ya timu kama Algeria, si kitu kidogo. Wazoefu kama Ngassa na wengine wapo, lakini ninaamini tutapambana.


SALEHJEMBE:Mwisho kwa Watanzania wapenda soka, una lolote la kuwaeleza?
Mkwasa: Sisi tuko hapa tunapambana sana, natamani wangeona kila jambo. Nia yetu ni kupigania taifa la Watanzania, nao wakiwa ndani. Hivyo siku hiyo waje, vijana wakiona watu wanawaunga mkono nao wataongeza juhudi zaidi, watajua wana deni. Nawakumbusha sisi tunafanya kazi kwa niaba yao Watanzania. Waje kwa wingi tuungane kupambana na Waalgeria ambao watakuwa wakitusubiri kwao kuungana na mashabiki wao ili watuchanganye.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic