July 22, 2016

TAMBWE (KULIA) AKIKABIDHIWA TUZO YA MFUNGAJI BORA NA MOHAMMED HUSSEIN DAIMA MAARUFU KAMA MMACHINGA.

Baada ya kukabidhiwa Tuzo ya Ufungaji Bora wa Ligi Kuu Bara 2015/2016, straika wa Yanga, Amissi Tambwe amefunguka kuwa siri kubwa ya mafanikio yake uwanjani ni kujituma na kutumia akili kufanya maamuzi na kudai kuwa hana imani na masuala ya kishirikina.

Tambwe alikabidhiwa tuzo hiyo baada ya kufunga mabao 21 na kuonyesha kuwa ana uwezo mkubwa wa kufunga kwa kuwa amekuwa akifanya hivyo tangu alipokuwa akiichezea Simba.

“Mafanikio yangu wala hakuna juju (ushirikina), siri kubwa ni kujituma kwangu na kuwazidi akili mabeki wengi hawa wa kwenye ligi kuu.

“Unajua mabeki wengi wa hapa Tanzania wanatumia nguvu nyingi kunikaba, pia wananipania sana, hivyo mimi ninachofanya ni kucheza kwa ujanja na kutumia akili nyingi.

“Mbinu nyingine ninazozitumia ni kucheza na eneo la ndani ya boksi la timu pinzani kwa ajili ya kusubiria pasi za mwisho, krosi na kona kutoka kwa mawinga na mabeki wetu wa pembeni ambao ni wazuri kwa kupiga mipira hiyo,” alisema Tambwe.

Kuhusu kutong’ara kimataifa, Tambwe alisema huko anakutana na mabeki wengi wanaotumia akili nyingi na uzoefu wa kukaba, hali inayosababisha apate ugumu wa kufunga mabao.

Aidha, aliongeza kuwa kuongezeka kwa majukumu uwanjani kama anavyoagizwa na kocha wake, Hans van Der Pluijm kucheza namba 10 tofauti na mwanzoni alikuwa akicheza namba 9, kumesababisha kasi yake ya kufunga mabao kupungua.

SOURCE: CHAMPIONI


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic