January 2, 2020



MZUNGUKO wa kwanza bado unaendelea kwenye Ligi Kuu Bara ambayo kwa sasa imezidi kuwa na ushindani kutokana na kila timu kusaka ushindi ndani ya uwanja.

Kuna mengi ambayo yanatokea ndani ya uwanja na nje ya uwanja ni muhimu kujifunza na kuongeza ubora zaidi kwa yale ambayo yamepita na yale ambayo yanaendelea kwenye soka letu la Bongo.

Pongezi kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa kuweza kuweka usawa kidogo katika ratiba msimu huu kwa kuwa hakujawa na viporo vingi labda ni kwa sababu msimu huu timu zetu zimeishia hatua ya awali kwenye Ligi ya Mabingwa hii ni mbaya kwetu kwa msimu huu kwa kushindwa kupenya kimataifa.

Kwa mapenzi ya Mungu tumeweza kuonana tena ndani ya mwaka mpya 2020 ni jambo la kushukuru kwa kweli kwani yeye ndiye anayetulinda na kutupigania hivyo tunapaswa tushukuru kwa yote ambayo yametokea kwa mwaka uliopita.

Maumivu makubwa ambayo tuliyapata mwaka jana 2019 hasa kwa upande wa kimataifa kwa kuwa hakuna timu iliyofanya vema zote ziliboronga jambo ambalo limetufanya tuwe na usimanzi mwaka huu mambo yawe mengine kabisa ya kutafuta mafanikio.

Timu yetu ya Taifa chini ya miaka 17, Serengeti Boys iliboronga kwenye michuano ya Cecafa iliyoandaliwa na TFF ni jambo baya kwetu kulirudia tena ama kulisahau bila kulifanyia kazi kwa kutafuta majibu yake mwaka huu mpya.

Yale makosa ambayo yalitukosesha furaha mwaka uliopita tuachane nayo tutafute majibu sahihi ambayo yatatufanya tuwe imara muda wote kwenye michuano ambayo tunaandaa ama kualikwa na kufanya kweli ndani ya mwaka 2020.

Hakuna kukumbuka mafanikio kisha ukadhani utafanikiwa muda wote ndani ya mwaka 2020 bila kutafuta majibu kwa yale uliyofeli itakuwa ni uongo wa karne hivyo kwenye soka haupaswi kupewa kipaumbele.

Tusisahau kwamba hata timu ya Taifa ya Wanawake, Kilimanjaro Queens nayo pia iliboronga ikiwa nyumbani kwa kushindwa kuifunga Kenya kwenye mchezo wa fainali wa Cecafa iliyofanyika hapahapa Bongo tena uwanja wa Chamazi na lundo la mashabiki.

Katika yale makombe ambayo tulikuwa wenyeji msimu uliopita tuliboronga na kuweka rekodi mbovu ambayo inapaswa sasa itafutiwe majibu ndani ya mwaka 2020 ambao tumeanza ukurasa mpya.

Michezo mingine ambayo imekuwa ikitubeba imekuwa haipewi kipaumbele kikubwa licha ya watanzania kupambana kufanya vizuri ni wakati wa kutazama nini tutafanikiwa kuinua zaidi ya pale tulipokuwa.

Hapo kuna mchezo wa ngumi ambao umeanza kurejea kwenye ubora wake ni muda wa kutazama namna gani tunaweza kufikia malengo ya kuwa juu kuliko hapa tulipo.

Yale mazuri ya TFF yanapaswa yaongezwe zaidi kwenye utendaji na kufanya utekelezaji ule unaoonekana kwani stori kwenye soka huwa hazijengi vitendo ndio kitu cha msingi katika hili.

Taifa linahitaji kuona kwamba hakuna mambo ya kuchanganya siasa na mpira kwa zama hizi zaidi ya kuangalia namna gani tunajipanga kuleta ushindani katika kile ambacho tunakifanya.

Wachezaji wana jukumu la kufanya tathimini ya kile ambacho walikifanya ndani ya uwanja kwa mwaka uliopita kama kinaendana na uwezo wao pamoja na timu ambayo wanaitumikia.

Mashabiki nao mwaka huu wanatakiwa wabadili mfumo wa ushabiki sio wanajitokeza uwanjani kuzomea pale wapinzani wao wanaposhindwa kufanya vizuri na kuishia kushangilia chenga na mabao kisha muda mwingine wanakaa kimyaa hii ni mbaya.

Kila mmoja afanye kazi kwa umakini na kwa wajibu kwa mwaka huu nina amini ndugu msomaji itakuwa rahisi kuyafikia malengo ambayo tumejiwekea kiujumla kwenye uwanja wa soka letu.

Sasa ngoja twende kule ambako nilikuwa nimelenga leo kuzungumzia kwa upana ni kuhusu ushindani uliopo kwenye Ligi Kuu Bara ambayo inaendelea kwa sasa.

Hali halisi tunaiona kwa sasa jambo ambalo limepamba moto ni mchezo wa watani wa jadi ambao ni  Simba na Yanga utakaochezwa uwanja wa Taifa.

Tayari vuguvugu limesambaa na kila kona ni wimbo mmoja tu mechi ya Simba na Yanga ambazo zitapambana ndani ya uwanja hivi karibuni na kuendeleza mchezo wa ligi.

Kila timu inapambana kwa namna inavyoweza kuweza kujiweka rekodi yake ndani ya mwaka mpya wa 2020 kwenye mechi zao za mwanzo jambo jema kusaka ushindi wa halali na sio ujanjaujanja.

Hakuna mwalimu duniani ambaye anaingia Uwanjani akiwa anafikiria kufungwa, sasa kama ipo hivyo basi hata mbinu za kutafuta ushindi zinapaswa zibadilike.

Tunahitaji kuona soka safi na kila mchezaji ndani ya uwanja aonyeshe sababu ya kuwa ndani ya Yanga ama Simba na sio kumtegemea mchezaji fulani ndiye ataokoa jahazi hakuna kitu hicho kwa sasa.

Sasa ni wakati mwingine wa kukaza buti na kutumia akili na nguvu kutafuta matokeo chanya kwenye michezo yote ya ligi ikiwa ni pamoja na huu utakaochezwa Jumamosi ambao utavuta hisia za wengi zaidi.

Uzuri ni kwamba mshindi wa mechi hii hatabiriki haijalishi nani yupo vizuri kifedha ama kitimu hakuna kinachomata katika mechi hii zaidi ya kuangalia maandalizi halisi ya wachezaji.

Ushindani ukiwa mzuri ni nafasi yetu hasa kutengeneza timu bora ya Taifa hasa na kufanikiwa kuibua vipaji ambavyo ni kwa manufaa yetu wenyewe.

Tuna wachezaji wa kigeni ambao wanafanya vizuri hao wawe ni chachu kwetu kuongeza juhudi na kuonyesha uwezo ambao tunao na sio kukimbilia kubeza uwezo wao.

Mwalimu anapenda kumtumia mchezaji mwenye kubadilisha matokeo muda ambao hakuna shabiki anayeamini kwamba kuna jambo litatokea.

Hicho ndicho ambacho mchezaji anapaswa afanye hasa akiwa uwanjani, juhudi zake na kujituma ni faida kwa timu nzima na sio yeye peke yake.

Muda mwingine timu inapata matokeo mabovu kutokana na kuamini uwepo wa mchezaji fulani ndani ya kikosi utatusaidia hali inayoleta shida wakati akiwa hayupo.

Wengi bado hawajajua maisha ambayo tunaishi tunayabeba kwa asilimia kubwa kwenye saikolojia na maisha yetu hivyo mfumo wetu unavyofikiria kuna jambo fulani litatokea ndivyo inavyokuwa.

Wachezaji wote ni muhimu hakuna ambaye ni bora kuliko mwingine zaidi kinachotofautisha ni nafasi na ule uwezo binafsi wa kulazimisha mambo yatokee Uwanjani.

Basi kama yote yanawezekana kuna haja ya kufanya mabadiliko makubwa ndani ya uwanja na nje ya Uwanja kwa kuamini kwamba kila mchezaji ana nafasi ya kubadilisha matokeo akiwa ndani ya uwanja.

Mashabiki watakaojitokeza wasiwe na matokeo mikononi mwao hilo litawatesa na kuwaumiza baadaye ndani ya dakika tisini ndipo ninaamini mshindi atapatikana ama kama itakuwa ngoma sare hapo ndipo tutapata ukweli wa mambo.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic