May 1, 2021


 MUDA mgumu na mbaya ambao huwa unachukiwa na baadhi ya watu ni ule wa  kupanda, kwani kunakuwa na shida nyingi shambani huku usingizi nao ukiwa unaendelea kubembeleza kwa wale ambao wanahitaji kwenda shamba.

Ipo hivyo siku zote maisha yetu yametawaliwa na uzembe mwanzo ila mwisho ambapo kunapatikana mavuno basi hapo huwa kuna aina mbalimbali za tabasamu ambalo linapatikana.

Wapo ambao huwa wanatabasamu kwa kufurahia kile wanachokipata huku wengine wakiamini hawastahili kukipata hicho wanachokivuna na kusahau kwamba yote yalitengenezwa awali wakati wa kupanda.

Nadhani mwanafamilia ya michezo unaweza ukadhani nimeamua kukuacha, hapana nipo nawe na ninazungumzia michezo kama ilivyo kawaida.

Shamba ambalo linazungumziwa hapa ni ule uwezo na jitihada za mchezaji kuonyesha kile ambacho kiliwafanya mabosi wake wampe dili la kusaini katika timu ambayo anaitumikia.

Ikiwa atakuwa anaona uvivu kujituma na kuonyesha uwezo wake inakuwa ngumu kwake kupata mavuno makubwa hasa wakati ule mkataba wake unapoisha ama muda mwingine kupata ofa kwenye timu nyingine.

Imekuwa bahati mbaya wachezaji wengi wamekuwa wakipata nafasi wanashindwa kuzitumia na kuishi kwenye maisha yale ambayo waliishi jana na kusahau kwamba siku hazigandi zinakwenda mbele.

Kwa wale ambao bado wanaona uvivu kupanda mbegu bora shambani wakati wa mavuno unakaribia hivyo ni jukumu lao kushtuka mapema na kupanda mbegu bora ambayo ni jitihada.

Kufanya kwao vizuri ndani ya uwanja ni muda wao wa kuwa sokoni na itawafanya wafurahie mavuno ambayo ni timu mpya pamoja na dau lao kuwa kubwa.

Ipo wazi kwamba mzunguko wa pili ukikamilika kuna wachezaji watapewa mkono wa kwa heri na wengine muda wao kuishi ndani ya Ligi Kuu Bara utakuwa umekwisha hivyo tutakutana nao Ligi Daraja la Kwanza.

Ipo wazi kuna timu ambazo zitashuka basi kwa wachezaji ni muda wao kupambana ili wapate fursa kuendelea na maisha yao kwenye ligi ama mabosi wa hizo timu ambazo zitashuka wakubali uwezo wao waanze nao maisha ndani ya Ligi Daraja la Kwanza.

Kupata kazi ni kitu kizuri na kupoteza pia kazi ni kitu kizuri kwa kuwa itakufanya upambane ili upate kazi nyingine sasa kama timu itashuka nina amini kwamba wachezaji nao wana kazi ya kufanya kujitoa hapo walipo.

Imani yangu ni kwamba mchezo wa mpira muda mwingi namba zinazungumza na kwa wale ambao wamekwama kufanya vizuri wakati huu muda wao wa kupewa mkono wa kwa heri unakuja.

Ikiwa mchezaji utapata nafasi ya kupambana muda huu fanya vizuri. Unaweza ukasema mbona zimebaki mechi 7 ama 10 bado hizo kwenye ulimwengu wa mafanikio ni nyingi na mechi moja inaweza kubadili upepo wa maisha yako kutoka daraja moja kwenda lingine.

Nina mifano ya kutosha kwa wale wachezaji ambao timu zao ziliposhuka wao waliendelea na maisha kwenye ligi na wengine waliendelea na maisha kwenye timu hizo Ligi Daraja la Kwanza.

Yote hayo yalitokana na jitihada zao, hawakuwa wavivu bali ni wale wenye juhudi isiyokuwa ya kawaida katika kutafuta matokeo.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic