July 21, 2021

OFISA Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), Almas Kasongo, ametangaza neema kwa timu 16 zitakazoshiriki Ligi Kuu Bara msimu ujao wa 2021/22 kupitia mikataba ya udhamini wanayotarajia kuiingia hivi karibuni.

Kasongo amesema baada ya kumaliza mkataba na kampuni ya Vodacom waliokuwa wakiidhamini ligi hiyo, hivi sasa wapo kwenye mazungumzo ya mwishomwisho na kampuni tatu tofauti zilizo tayari kuweka mzigo wa maana kwenye udhamini.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Kasongo amesema kampuni ambazo wapo nazo kwenye mazungumzo, moja ni ya ndani ya nchi na mbili ni kutoka nje lakini zinafanyia kazi zake hapa nchini.

“Vodacom wamemamliza mkataba wa kuidhamini ligi yetu, tunawashukuru kwa muda wote tuliokuwa nao kwani walitushika mkono kwa takribani miaka 20 kuanzia mwaka 2002.

“Baada ya wao kumaliza mkataba kwa sasa, kuna makampuni matatu ambayo tupo nayo kwenye mazungumzo yanayoenda vizuri, imani yetu ni kwamba kabla ligi haijaanza, tutasaini mkataba na mojawapo ambayo ndiyo itakuwa mdhamini mkuu.

“Kwa kuwa mtoto (Ligi Kuu) anakuwa, hivyo dau pia nalo litakuwa kubwa zaidi, hivyo tusubiri muda ufike mambo yatakuwa hadharani.” Amesema Kasongo.

 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic