August 7, 2015


Mabingwa wapya wa Kombe la Kagame ni Azam FC, hii wala sia hadithi mpya na tutaendelea kusema hongera kwao.
Utaona kuna ambao hawajapenda mfano wale Wakenya ambao walikuwa wakisambaza maneno ya uzushi kwenye mitandao, kwamba Azam FC imenunua ubingwa.


Kawaida ni watu wenye husda, wasioamini Tanzania inaweza ikafanya jambo bora. Kikubwa kama nilivyoeleza awali ni kuwapuuza.
 
Mmoja wa viongozi ambao wamekuwa wakijitahidi kusaidia michezo nchini ni Rais Jakaya Mrisho Kikwete. Ameonyesha hilo kwa dhati mbele ya wapenda soka, kikapu, netiboli na michezo mingine.

Serikali yake, haina mapenzi ya wazi na mchezo wa soka. Unaweza kusema imejitahidi lakini hakuna mpangilio mzuri wa kusaidia soka na michezo mingine.

Siku chache zimepita tokea Azam FC ilipofika Ikulu kwenye kumuonyesha Kombe la Kagame Rais Kikwete. Kombe ambalo wamelibeba kwa historia ya aina yake.
Azam FC imebeba kombe hilo kwa mara ya kwanza bila ya kupoteza hata mchezo mmoja, timu iliyobahatika kuepuka kipigo ndani ya dakika 90 ni Yanga pekee ambayo walikutana nayo kwenye robo fainali.
 
Wakati wanamkabidhi kombe hilo Kikwete aliwaeleza mambo kadhaa, lakini moja ulikuwa ni msisitizo wake kuhusiana na suala la kuhakikisha hawaishii Afrika Mashariki na Kati.
Kikwete aliwaeleza Azam FC mambo mengi kadhaa ambayo ni muhimu sana kuhusiana na suala la walipofikia na likiwemo lile na kutokubali kuwa matawi ya YAnga na Simba.

Hawajawa matawi, wamekuwa washindani ndiyo maana leo wamefikia hapo na huenda wana nafasi nzuri ya kufika mbali zaidi ya hapo.
 
Maneno ya Kikwete kwamba Azam FC wasione wamefika kwa kutwaa ubingwa wa Kagame ni jambo bora ambalo linapaswa kubaki kwenye vichwa vya viongozi, wachezaji na hata mashabiki.

Azam FC imeanza vizuri, imefikia sehemu nzuri na inaweza kufika zaidi ya hapo ilipo lakini kama itakuwa na watu wanaotaka kweli kupiga hatua na kufikia mbali.

Afrika ndiyo nyumbani kwa Azam FC, mafanikio yanaweza kupatikana kwa kiwango cha juu kama ushindani utatangulizwa na klabu hiyo itajiamini inaweza kufika.

Kikubwa kusimamia malengo, kwamba uongozi unataka ambacho umekianzisha. Ujiamini kwamba unaweza kufanya zaidi ya zilivyofanya Yanga na Simba.
 
Hakuna ubishi itahitaji muda kwa kuwa Yanga na Simba ni wakongwe, wametokea mbali. Lakini miaka kumi ijayo, Azam FC itaanza kuhesabu pia imetoka mbali.

Huenda utakuwa pia ni wakati mzuri wa kuanza kupiga hesabu ya mafanikio yake, imechukua vikombe vingapi na imefikia wapi.

Hivyo, muda hausubiri, maneno ya Kikwete yabaki kama chachu ya kuikumbusha Azam FC kwamba haijafika na haipaswi kuwa na woga hata kidogo. Hivyo iendelee kupambana hadi kieleweke.







0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic