TIMU ya Sevilla inatarajiwa kuwasili nchini Tanzania kesho Jumanne kwa ajili ya mchezo wa kirafiki ulioandaliwa na Kampuni ya SportPesa kwa ushirikiano wa La Liga.
Sevilla inatarajiwa kucheza mchezo huo wa kirafiki na Mabingwa wa Ligi Kuu Bara utakaopigwa Alhamisi ya wiki hii kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam saa moja kamili usiku.
Akizungumza na Waandishi wa Habari, Mkurugenzi wa Utawala na Udhibiti SportPesa Tanzania, Tarimba Abbas amesema “SportPesa inakwenda kuweka historia kwa mara nyingine tena nchini kwenye sekta ya soka kwa kuileta timu ya kimataifa ya Sevilla.
“Kupitia ujio wa timu ya Sevilla watafanya shughuli mbalimbali zenye lengo la kuinua sekta ya michezo nchini kwa vijana na soka kwa ujumla.
“Watatoa mafunzo ambayo yatahudhuriwa na timu ya vijana ya Bom Bom FC kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar bila kusahau semina elekezi itakayotolewa na maofisa wa klabu ya Sevilla kwa viongozi wa klabu, TFF na washirika wake ili wapate kuimarika kitaaluma na kupata uelewa jinsi ya kuongeza mapato,”amesema Tarimba.
Naye Mkurugenzi wa Mashindano wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Salum Madadi amemtaja mwamuzi wa kati wa kimataifa wa Tanzania, Herry Sassi ndiye aliyeteuliwa kuchezesha mchezo huo atakayesaidiana na Mohamed Mkono (Tanga), Soud Lila (Dar) huku mwamuzi wa akiba akiwa ni Jonesia Rukyaa (Kagera).
“Waamuzi wanaochezesha mchezo huu wote ni waamuzi wenye beji ya Fifa, mchezo huu mbali ya kujitangaza kama nchi lakini pia ni sehemu ya kutangaza vitu vyetu mbalimbali wakkiwemo wachezaji na waamuzi wetu,”amesema Madadi.
Kwa upande wa Simba, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa timu hiyo, Haji Manara amesema kuwa “Bado tunaendelea kuwashukuru SportPersa kwa kufanikisha ujio wa Sevilla nchini, ni fursa ambayo kila timu ya soka Afrika ingetamani kuipata.
“Maandalizi ya mchezo huo na Sevilla yanaendelea vizuri, timu imeelekea Singida kwa ajili ya mchezo wa Ligi Kuu Bara tutakaocheza kesho huko Namfua na mara baada ya mchezo huo timu itarejea kwa ajili ya kujiandaa na pambano hilo,”amesema Manara.
|
0 COMMENTS:
Post a Comment